TRA

TRA

Tuesday, January 26, 2016

Hongera Mkurugenzi TBS kwa uchapakazi

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !
















Kulia ni Joseph Masikitiko akizungumza katika moja ya mikutano yake..

Julian Msacky

MAPEMA mwezi huu shehena ya mafuta ya petroli yenye ujazo wa tani 38,521 ilikamatwa nchini baada ya kubainika kuwa mafuta hayo yalikuwa hayafai kwa matumizi.

Shehena hiyo ni kubwa, lakini jambo la kujifunza hapa ni kwamba zipo bidhaa nyingi ambazo zinachangia kusababisha madhara kwa Mtanzania tena ya kujitakia.

Kama mfanyabiashara anaamua kuingiza nchini mafuta yasiyo na ubora maana yake hathamini maisha ya wengine. Mafuta yake yakisababisha ajali si tatizo ili mradi apate fedha.

Hii si sahihi hata kidogo. Ni kukosa ubinadamu. Kimsingi wanaofanya biashara za aina hiyo wanatakiwa kutazamwa mara mbilimbili kwa sababu hawana nia njema na wengine.

Ni kwa msingi huo ninashauri uroho wa fedha usifikie hatua ya kugharimu hata maisha yetu. Kuingiza mafuta yasiyofaa athari zake kwa vyombo vya moto ni kubwa mno.

Miongoni mwa athari hizo ni mitambo ya magari kuharibika na hivyo kutoa fursa au nafasi kubwa ya vyombo hivyo kusababisha ajali na kupoteza maisha ya watu wasio na hatia.

Ifahamike kuwa shehena hizo zilikamatwa Bandari ya Dar es Salaam kwenye meli ya MT. Ridgebury John B kutoka Falme za Kiarabu ambao ni waagizaji.

Hata hivyo, yalizuiliwa kwa kukosa viwango vya ubora kwa mujibu wa Sheria ya Viwango Namba 2 ya 2009. 

Ni kwa msingi huo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Joseph Masikitiko anasema kukamatwa kwa shehena hizo kunatokana na ukaguzi uliofanywa na wataalamu waliobobea, wakiwemo wa mafuta na maabara.

Kwa mujibu wa Masikitiko ubora wa mafuta ya petroli hupimwa kwa kutumia kiwango namba TZS 672:2012/EAS 158:2012 ambacho kimeoanishwa kwa kuzingatia matakwa ya nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki.

Masikitiko anasema matakwa hayo ni pamoja na kuhakikisha yanafaa kwa matumizi ya magari, afya ya wananchi na uhifadhi wa mazingira. 

Hata hivyo, alisema mafuta hayo hayakukidhi viwango kwani yana uwezo mkubwa wa kuvuta maji au mvuke, jambo ambalo si zuri.
Mkurugenzi huyo anasema mafuta ya aina hiyo hayawezi kufanya kazi iliyokusudiwa katika injini kutokana na uwepo wa maji katika petroli.

Anasema mvuke ukiwa mwingi kwenye injini husababisha mtiririko wa mafuta kwenda kwenye injini kutokuwa mzuri na kisha kuiharibu.

Pia, mafuta ya aina hiyo husababisha kupungua kwa nishati ya kuendeshea injini hivyo, kuharibika haraka kwani wingi wa ujazo wa mafuta usiokuwa na uhalisia hutoa nishati isiyolingana na wingi wake.

"Madhara yake ni mnunuzi kununua na kulipa wingi wa mafuta usio na thamani halisi, pia huongeza uharibufu wa mazingira kutokana na moshi mchafu wa mitambo unaotoka kwenye magari,"anasema.

Alisema madhara mengine ni kiuchumi kwani, nchi hulazimika kutumia fedha nyingi za kigeni kuagiza vipuri kwa ajili ya matengenezo ya magari mara kwa mara. 

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo athari nyingine husababisha uchumi wa mtu binafsi kuyumba kutokana na kutumia gharama nyingi kutengeneza injini na vipuri vyake. 

"Benzene ikizidi kwenye mafuta ya petroli husababisha ugonjwa wa kansa, hasa kwa wale wanaotoa huduma za uuzaji wa petroli," anasema.

Ni kutokana na athari hizo na nyingi nyingi tunashauri wafanyabishara wetu wawe waaminifu katika shughuli zao hususan kununua bidhaa zenye ubora.

Bila kufanya hivyo maisha ya wananchi wetu yataendelea kuwa hatarini kila siku. Ninajiuliza kama shirika hilo halikukamata mafuta hayo si yangeingia sokoni?

Kama yangeingia kwenye mzunguko athari zake bila shaka ni nyingi. Ni kwa msingi huo tunaamini hata ajali zinazotokea mara kwa mara nchini yapo mambo mengi yaliyofichika.

Ni wakati muafaka kwa shirika hilo kuongeza nguvu katika ukaguzi ili kubaini bidhaa nyingine za vyombo vya moto ambazo zinaingizwa nchini kwetu kinyemela.

Inawezekana vifaa vingi vinavyofungwa katika vyombo hivyo, yakiwemo matairi hayana ubora unaotakiwa na hivyo kuwa kitanzi kwa watumiaji.


Tunaendelea kulitia moyo shirika kufanyakazi zake kwa uaminifu ili kulinda maisha ya Watanzania kwa sababu ndilo linaloshikilia maisha yetu kwa asilimia kubwa.
Kwa msingi huo watendaji wake wanatakiwa kupatiwa nyenzo nzuri ili waweze kutimiza majukumu yao vizuri. Kwa kufanya hivyo watatuokoa na mambo mengi.
Jambo jingine ni waagizaji wa bidhaa kuwa na roho ya huruma kwa walaji. Wakiwa na roho ya huruma hawatakubali kuingiza nchini vifaa au bidhaa za ovyo ovyo.
Kama alivyosema Masikitiko bidhaa zisizo na ubora zinachangia umaskini kwa wateja. Hii ni kwa sababu wanapoteza fedha zao kununua vitu visivyodumu muda mrefu.
Matokeo yake wanaendelea kutoboa mifuko yao kila siku. Akinunua radio au simu zikipita siku chache tu matatizo yanaibuka na mara anaachana nayo.
Katika mazingira ya aina hii mteja au mnunuzi anageuka mwathirika wa kubeba msalaba wa bidhaa zisizofaa kwa matumizi, hivyo lazima tushikamane kuumbua wahusika.
Kuwaumbua ni wananchi kutoa taarifa katika mamlaka husika wanapoona au kuhisi vitu, vifaa au bidhaa wanazouziwa, yakiwemo mafuta yana matatizo.
Hebu fikiria hiyo ni shehena ya mafuta ya magari au mitambo. Ingekuwaje kwa mfano, mafuta hayo yalikuwa ya kupikia bila shaka maisha ya wengi wetu yangekuwa hatarini.
Si hivyo tu, lakini tunaamini yapo mafuta ya kula yanapenyezwa nchini na shirika kushindwa kubaini wahusika. Ndiyo maana siku hizi milipuko ya magonjwa imekuwa mingi mno.
Watu wananenepeana ovyo ovyo. Hili nalo linatakiwa kutazamwa kwa undani. Ni vema shirika likafungua macho zaidi ili kunusuru maisha ya wananchi wetu.
Hii ina maana kuwa watu wachache wasipewe nafasi ya kucheza na maisha ya Watanzania kwa sababu ya maslahi yao. Ni imani ya wengi wetu kuwa mchezo huo utakomeshwa leo au kesho.




Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger