Serikali ya mpito ya Sudan Kusini iliyotarajiwa kuanza rasmi shughuli zake hii leo imetangaza kuakhirisha mpango huo.
Msemaji
wa serikali Atenya Wek Ateny, amethibitisha hayo na ameweka wazi kwamba
takriban thuluthi mbili ya masuala ya kiserikali yataendeshwa kama
ilivyokuwa huko nyuma. Serikali hiyo ya mpito ya Umoja wa Kitaifa
ilitarajiwa kuundwa leo (22.01.2016) ili kumaliza mgogoro wa miaka
miwili uliosababisha zaidi ya watu 15,000 kuuwawa kwa mujibu wa Umoja wa
Mataifa. Serikali ya mpito ya Umoja wa Kitaifa ilikuwa ikitarajiwa
kuundwa na kuanza kazi leo ikihusisha mawaziri 30.
Kuundwa
kwa serikali hiyo ni mchakato uliokwenda sambamba na makubaliano ya
amani yaliyotiwa saini na viongozi wawili wanaozozana Rais Salva Kiir na
makamu wake wa zamani Riek Machar kufuatia shinikizo la kimataifa mnamo
mwezi Agosti mwaka jana.
Vita vya
wenyewe kwa wenyewe vilivyosababisha watu zaidi ya milioni mbili
kuachawa bila makaazi vilihusisha mapambano kati ya wanajeshi wa
serikali ya Rais Kiir na waasi wanaomuunga mkono mpinzani wake kisiasa
Riek Machar.
Siku ya kihistoria
Kimsingi
leo ilikuwa siku muhimu iliyotarajiwa kuweka msingi wa kupigwa hatua
katika historia ya taifa hilo la Sudan Kusini ambalo limeshuhudia miaka
miwili ya mapigano kati ya pande hizo mbili hasimu.
Raia
zaidi ya milioni 12 wa nchi hiyo walitarajia kuiona serikali mpya ya
mpito itakayozijumuisha pande zote huku Salva Kiir akiendelea kushikilia
nafasi yake kama rais na Machar kurudishwa katika nafasi yake ya
zamani, yaani makamu wa rais.
Serikali
hiyo ya mawaziri 30 ikitarajiwa kwamba itajumuisha watu sita
walioteuliwa na Rais Kiir huku wengine 10 wakiteuliwa na Machar na
wawili wakiteuliwa kutoka upande wa wale waliokuwa wamezuiliwa jela na
wengine wawili wakiteuliwa na muungano wa vyama vidogo vya kisiasa
nchini Sudan Kusini.(P.T)
SHARE








No comments:
Post a Comment