TRA

TRA

Monday, April 24, 2017

MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA ALAANI VURUGU ZILIZOTOKEA KATIKA MKUTANO WA WANAOSEMEKANA KUWA NI VIONGOZI WA CUF NA WAANDISHI WA HABARI

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !


  Nimesoma na kuona katika vyombo mbalimbali vya habari kuhusu vurugu zilizotokea tarehe 22 Aprili, 2017 katika hoteli ya Vina, Mabibo hapa Dar es salaam, zinazosemekana kuhusisha wanachama wa CUF.

Ni ukweli usiopingika kuwa, suala la mgogoro wa uongozi katika chama cha CUF lipo mahakamani, lakini nikiwa msimamizi wa Sheria ya Vyama vya Siasa na kutambuliwa na jamii kuwa ni mlezi wa vyama vya siasa; nimelazimika kuwasihi wadau wa siasa hususani wanachama wa chama cha CUF, kutambua kwamba, kuwapo kwa shauri mahakamani siyo fursa ya kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani, kwani jambo hili ni uvunjifu wa sheria na linaleta sura mbaya kwa jamii.

Hivyo, ninalaani vurugu hizo, ambazo zilionekana kuvunja amani na utulivu na watu kuumizwa, tofauti na tunu zetu za taifa za amani na utulivu. Pia, nawaasa wanachama wa CUF pamoja na tofauti walizonazo, madhali masuala haya yapo mahakamani hebu tuheshimu utawala wa Sheria.

Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa na hata Jeshi la Polisi lipo kushughulikia malalamiko yoyote yanayohusu uendeshaji na shughuli za chama chochote cha siasa. Hivyo, hakuna haja ya wanachama wa chama cha CUF kukiuka taratibu za kuendesha chama hicho au kujichukulia Sheria mkononi.

Aidha, ninaviasa vyama vya siasa kuelewa kuwa havipo juu ya Sheria, vinapaswa kuheshimu na kufuata Sheria za nchi, ikiwamo kutunza amani na utulivu tulionao.

Mwisho, ninaomba vyombo vya ulinzi na usalama katika nchi yetu kulifanyia kazi tukio hilo, ili wahusika wafahamike na kuchukuliwa hatua za kisheria. Kwa upande wa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inayosimamia utekelezaji wa Sheria ya Vyama vya Siasa, haitasita kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa Sheria.


                                              Jaji Francis S.K. Mutungi                                
MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA
24 Aprili, 2017.

Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger