


BENKI ya NMB imetoa msaada wa
mabati, mbao, misumari pamoja na vifaa vingine mbalimbali vya kupauwa
madarasa mawili ya Shule ya Msingi Karume vyote vikiwa na thamani ya
shilingi milioni tano ili kuisaidia shule hiyo kuondokana na msongamano
wa wanafunzi kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa.
Akikabidhi msaada huo juzi, kwa
niaba ya Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Dar es Salaam na Zanzibar, Bi.
Vicky Bishubo, Meneja wa NMB Tawi la Temeke, Christine Lifiga alisema
msaada huo ni utaratibu wa kawaida ambao benki hiyo imejiwekea kurejea
faida kiasi fulani wanayoipata kwa huduma anuai za kijamii ikiwemo
elimu.
Alisema NMB imeguswa na hali ya
upungufu wa vyumba vya madarasa katika shule hiyo na kuamua kutoa msaada
huo utakaowezesha kukamilika kwa madarasa mawili yatakayopunguza
msongamano wa wanafunzi kwenye madarasa. “…NMB itaendelea kuunga mkono
juhudi za Serikali katika kuchangia huduma mbalimbali za kijamii ikiwemo
elimu pale inapokuwa na chochote,” alisema Meneja huyo wa NMB Tawi la
Temeke, Bi. Lifiga.
Kwa upande wake Kaimu Ofisa Elimu
Manispaa ya Temeke, Bakari Mnondwa aliishukuru Benki ya NMB kwa kuwa
mstari wa mbele kusaidia hali ya uboreshaji elimu maeneo mbalimbali
ikiwemo katika shule za manispaa hiyo. “…Kweli nyinyi ni wadau muhimu wa
maendeleo ya elimu, tunaomba muendelee kuwa na moyo huo huo wa kusaidia
Serikali katika uboreshaji elimu. Serikali ina mzigo mkubwa haiwezi
kuboresha kila jambo ndio maana mara zote tunawafuata wadau kama nyinyi
kusaidia kama mlivyofanya,” alisema Bakari Mnondwa.
Uboreshaji wa elimu unaofanywa na
Serikali kwa kushirikisha wadau kama NMB unasaidia kupunguza kero
mbalimbali na kuongeza ufanisi maeneo mbalimbali ya elimu, hivyo kuiomba
benki hiyo isichoke kusaidia pale inapoombwa. “..Jamani tunaomba
msituchoke nyie ni wadau wetu muhimu hivyo tuendelee kushirikiana,”
alisisitiza ofisa huyo.
Awali akisoma risala kabla ya
hafla ya kukabidhiwa msaada huo, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Karume,
Hillgard Lwambusha aliishukuru Benki ya NMB kwa kutambua na kuthamini
maendeleo ya elimu Tanzania kwa kile kuisaidia shule hiyo msaada wa
vifaa vya kupaulia madarasa mawili jambo ambalo litapunguza changamoto
ya upungufu vyumba vya madarasa.
“…Ndugu Mkurugenzi Mkuu wa NMB
taasisi yako mmeweza kututatulia moja ya changamoto katika kufanikisha
kuweka mazingira bora ya utoaji wa elimu bora na sio bora elimu kwa
kutoa vifaa ambavyo vitaezeka vyumba viwili vya madarasa,” alisema
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Bw. Lwambusha.



SHARE
No comments:
Post a Comment