Mwandishi Wetu, TJNCDF
Wagonjwa wengi wenye tatizo la shinikizo la damu hushindwa kufanya
mazoezi ya mwili kutokana na ukweli kwamba, yanalazimisha moyo kufanya kazi ya
ziada.
Wagonjwa wengi wa moyo wanapojaribu kufanya mazoezi, hukabiliwa na
uchovu pamoja na kushindwa kuongeza pumzi.
Dalili hizi huwafanya wengi wao kuishi bila kuushughulisha mwili, jambo
ambalo huathiri zaidi afya zao, mipango yao ya kiuchumi na ubora wa maisha kwa
ujumla.
Ingawa mazoezi hufikiriwa kuwa ni hatari kwa wagonjwa wenye maradhi ya
moyo, tafiti za hivi karibuni zinabainisha kuwa mazoezi ni muhimu sana kwa watu
wenye maradhi haya.
Tafiti za kitabibu zinaonesha kuwa, mazoezi huwasaidia wagonjwa wa moyo
kutumia hewa ya oksijeni vizuri na kwa faida.
Mazoezi pia huongeza mzunguko wa damu katika misuli mwilini na
hupunguza kiasi cha lehemu mbaya mwilini, uwezekano wa kupata magonjwa
yatokanayo na uvimbejoto, uwezekano wa kulazwa hospitalini mara kwa mara,
matumizi ya dawa na vifo vya mapema.
Hii ni kwa mujibu wa Julie Adsett na Robbie Mullins wa Chuo Kikuu cha
Teknolojia cha Queensland cha Uingereza, katika chapisho lao la ushahidi wa
kisayansi kuhusu faida za mazoezi kwa watu wenye maradhi ya moyo ya muda mrefu,
lililotolewa mwaka 2010.
Katika makala yake iliyochapishwa katika jarida la Chama cha Madaktari
wa Marekani (JAMA) toleo la 288(16) la mwaka 2002, Dk. Jonathan Myers (PhD) wa
kitengo cha magonjwa ya moyo katika Chuo Kikuu cha Stanford nchini Marekani,
anasema kwamba wagonjwa wapya wanaogunduliwa kuwa na shinikizo la damu,
wanapata nafuu haraka wanaposhiriki katika mazoezi.
Lakini wanaweka bayana kuwa kabla ya kuanza programu ya mazoezi, watu
wenye maradhi ya moyo wanahitaji kupata uchunguzi na uangalizi wa karibu wa
daktari bingwa. Wagonjwa hawa wanashauriwa kufanya mazoezi mepesi na wasitumie
muda mrefu sana.
Watu wenye matatizo ya moyo wanaweza kufanya mazoezi ya kutembea,
kukimbia taratibu na kuendesha baiskeli kwa mwendo mdogo. Watu hawa pia
wanaweza kufanya mazoezi ya kunyoosha misuli pamoja na kukunja na kukunjua
viungo vya mwili mara kwa mara.
Mambo ya kuzingatia
Inashauriwa kuepuka mazoezi yanayohusisha kubeba uzito mkubwa na
mazoezi kama vile pushapu. Pia ni vizuri kujiepusha na mazoezi katika sehemu zenye
baridi kali hasa nje ya nyumba au katika sehemu zenye joto kali sana.
Wataalamu wa tiba za mazoezi wanapendekeza kuanza kwa mazoezi mepesi na
taratibu, huku ukiongeza kadri siku zinavyokwenda na kwa kadri unavyoendelea
kujisikia vizuri. Simamisha mazoezi mara moja pale unapojisikia kuchoka,
kizunguzungu, moyo kudunda bila mpangilio, kifua kuuma, kichefuchefu au
kuishiwa pumzi.
Andika kwenye daftari dalili yoyote inayojitokeza, wakati ilipotokea na
aina ya mazoezi uliyokuwa unafanya wakati dalili hiyo ilipojitokeza. Mweleze
daktari wako kuhusu taarifa hizo pale utakapokwenda kupata ushauri au huduma za
kitabibu. Usifanye mazoezi kama hujisikii vizuri au kama ulikuwa mgonjwa sana
katika siku za karibuni.
Kabla ya kufanya mazoezi pima mapigo yako ya moyo na kama yako zaidi ya
100 kwa dakika katika hali ya kupumzika, usifanye mazoezi na badala yake nenda
kamuone daktari kwa ushauri wa kitabibu.
Kama mapigo ya moyo yatakuwa sawa kabla ya mazoezi, unatakiwa kupima
tena baada ya mazoezi mepesi na kuona kuwa mapigo ya moyo yanarudi katika hali
ya kawaida ndani ya dakika kumi baada ya kusimamisha mazoezi.
Usifanye mazoezi muda mfupi baada ya kula. Subiri angalau zipite dakika
90 ndipo ufanye mazoezi. Ili kupata faida zaidi, fanya mazoezi unayoyapenda,
yanayokufurahisha na yasiyo kupotezea mapato yako.
Mazoezi ni nini?
Mzoezi siyoi lazima kwenda kwenye vituo maalumu vya mazoezi. Wataalamu
wa afya wanaeleza kuwa jambo lolote ambalo mtu atafanya kwa kuushughulisha
mwili wake kwa kusababisha viungo vifanye kazi na hata kumsababishia atoke
jasho linatafsiriwa kuwa ni sehemu ya mazoezi.
Kwa sababu hiyo wanayataja baadhi ya mambo ambayo yanaweza kuwa sehemu
ya mazoezi kuwa ni kazi za kutoa jasho, kutembea, kukimbia kukimbia, michezo au
mazoezi kulingana na wataalamu.
Baadhi ya mambo ambayo watu wanafanya na ikawa ni sehemu ya mazoezi ni
kama vile kuendesha baskeli, kutembea, kulima pamoja na kazi nyingine zinazotoa
jasho.
Hata hivyo, wataalamu wa afya wanashauri wenye matatizo ya moyo
wanapaswa kufanya mazoezi kwa maelekezo na usimamizi wa mtaalamu wa afya mwenye
taaluma kuhusu magonjwa ya moyo.
Makala haya yameandaliwa
na Chama cha Waandishi wa Habari Wanaopambana na Magonjwa Yasiyo ya Kuamukiza
(TJNCDF) kwa kushirikiana na Chama cha Ugonjwa wa Kisukari Tanzania (TDA).
Maoni au maswali tuma TJNCDF, S.L.P 13695, Dar es Salaam au tjncdf@gmail.com
SHARE
No comments:
Post a Comment