Rais wa
Ujerumani Joachim Gauck, hatagombea awamu ya pili ya miaka mitano
madarakani, ikizingatiwa umri wake na sababu za kiafya. Hayo
yameripotiwa na gazeti la Bild Ijumaa (03.06.2016)
Gauck,
mwenye umri wa miaka 76, anatarajiwa kutoa maelezo juu ya uamuzi wake wa
kutowania muhula wa pili kama mkuu wa dola katika mkutano na kansela wa
Ujerumani Angela Merkel siku ya Jumatatu, gazeti hilo liliripoti.
Gauck
anatarajiwa kutoa tangazo rasmi kwa umma siku ya Jumanne mjini Berlin.
Muhula wa Gauck, unakamilika Machi 2017. Msemaji wa rais huyo amekataa
kutoa kauli kuhusu suala hilo. Rais Gauck aliidhinishwa kuwa rais Machi
2012, kuchukua nafasi iliyoachwa na Christian Wulff, ambaye baada ya
miezi 20 tu alilazimika kujiuzulu kutokana na kashfa iliyohusisha mkopo
wa nyumba.
Mwaka
2010 Gauck alishindwa na rais wa zamani Wulff wakati alipokuwa mgombea
wa muungano wa vyama vya Kijani na Social Democratic, SPD. Mwaka 2012
kansela Merkel na muungano wa vyama ndugu vya Christian Democratic
Union, CDU na Christian Social Union, CSU, ulimuunga mkono Gauck baada
ya mabishano kadhaa.
Mwezi
uliopita viongozi wa vyama vinavyounda serikali viliahidi kuunga mkono
muhula wa pili wa rais Gauck. Gazeti la Frankfurter Rundschau liliripoti
kwamba chama cha Christian Democratic Union, CDU cha kansela Merkel
pamoja na mshirika wake serikalini, chama cha Social Democratic SPD,
vilihofia athari za Gauck kukataa kugombea awamu ya pili.
Kwa
mujibu wa ripoti hiyo, uamuzi huo ungekwamisha kampeni zao za uchaguzi
wa shirikisho mwaka 2017, iwapo vyama havitoweza kukubaliana kuhusu
mgombea mmoja. Baraza maalumu linalomchagua rais litakutana Februari 12
mwaka ujao 2017.
Wajerumani wataka Gauck aendelee
Matokeo ya kura ya maoni ya hivi karibuni, yanaonyesha asilimia 70 ya Wajerumani wangependelea Gauck aendelee kuwa rais.
Rais wa
Ujerumani ni mkuu wa dola na kwa kiwango kikubwa hushikilia wadhifa wa
heshima, kuiwakilisha nchi katika masuala ya sheria za kimataifa na
mikutano rasmi.
Rais
hachaguliwi moja kwa moja na umma, bali huchaguliwa na kamati maalumu
inayowajumuisha wabunge wa bunge la Ujerumani, Bundestag, na idadi sawa
na hiyo ya wajumbe kutoka kwa mabunge ya mikoa.
Rais wa
Ujerumani huwa na muhula wa miaka mitano na anaweza kuchaguliwa tena
mara moja tu. Raia yeyote wa Ujerumani mwenye umri wa zaidi ya miaka 40,
anaweza kugombea urais. DW
SHARE








No comments:
Post a Comment