TRA

TRA

Monday, April 25, 2016

Demokrasia ni gharama

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !


Demokrasia yetu
imefungwa pingu


Julian Msacky

UCHAGUZI nchini Chad umemalizika na Rais Idriss Deby aliyeingia madarakani tangu mwaka 1990 ameendelea kushikilia nafasi hiyo kwa mwendo mdundo.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Chad (CEN) ilisema Rais Deby alipata asilimia 60 ya kura na mpinzani wake, Saleh Kebzabo aliambulia asilimia 12 ya kura.

Kwa mujibu tume hiyo idadi ya wapiga kura katika uchaguzi huo wa Aprili 10 ilikuwa milioni sita.

Kama kawaida ya chaguzi nyingi za Afrika, matokeo yaliyompa ushindi Rais Deby yalipingwa vikali na wapinzani, akiwemo Kebzabo.

Miongoni mwa malalamiko ya wapinzani ni kwamba kura zilichakachuliwa kwani mamia ya masanduku ya kura yalipotea, hivyo uchaguzi haukuwa huru na haki.

Hiki ni kilio cha muda mrefu kutoka wapinzani waliopo katika Bara la Afrika. Swali ni je, ni kweli wanachezewa mchezo mchafu au wanaamua tu kudeka?

Hii ni mada ya kujitegemea, hivyo leo tuendelee kujadili mada yetu ya viongozi kusigina demokrasia.

Wakati wapinzani wakilalamikia ushindi wa Rais Deby anayetokea Chama cha Patriotic Salvation Movement (MPS), Umoja wa Afrika (AU) ulisema ulikuwa huru.

Ninachotaka kusema hapa ni kuwa tangu Afrika ikumbatie mfumo wa vyama vingi, hakuna uchaguzi uliofanyika bila malalamiko au vurugu.

Tumeona na kushuhudia namna chaguzi zetu zinavyogubikwa na utata, zikiwemo vurugu, umwagaji damu, raia kukimbia nchi na mengine mengi.

Hii ina maana gani kwa Afrika? Maana yake ni kuwa tulikubali kupokea mfumo wa vyama vingi kwa shingo upande ili kufurahisha wanaotupatia misaada. 

Katika mazingira hayo hakuna kiongozi anayeangalia ameingia madarakani kwa kura halali au kwa kuua ili mradi tu aingie Ikulu kwa gharama yoyote.

Kwa lugha nyingine ni kuwa demokrasia katika chaguzi zetu inakuwa haina mwenyewe na badala yake mabavu na kejeli ndizo hutawala chaguzi zetu.

Ndiyo maana demokrasia katika nchi za Afrika ni kana kwamba imefungwa pingu ili kuruhusu wanasiasa uchwara na wababaishaji waendelee kutamba.

Tunadhani ni muda muafaka sasa kuruhusu demokrasia ifanyekazi badala ya kushikilia viongozi madarakani kwa silaha nzito nzito kana kwamba tupo vitani.

Viongozi wetu ni lazima wafahamu kuwa wananchi wamechoshwa na tabia ya kuchezea demokrasia kwani madhara yake yameonekana wazi wazi barani kwetu.

Badala ya kutumia muda wetu kufanya shughuli za maendeleo tunapoteza nafasi kubwa kujadili namna ya kurejesha amani iliyovurugwa na uchaguzi.

Katika bara letu hakuna mwenye uhakika uchaguzi unapomaliza kama watu wataendelea kuwa na amani au wataamshwa nyumbani na milipuko ya risasi.

Mathalan, kumalizika kwa uchaguzi wa Chad hakuna mwenye kujua kama amani na utulivu utakuwepo au la maana wapinzani bado wana kinyongo moyoni.

Aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dk Koffi Annan aliwahi kusema chimbuko la migogoro barani Afrika ni demokrasia duni.

Hii ikiwa na maana kuwa Afrika imepanda demokrasia yake kwenye mwamba. Kwa msingi huo haistawi zaidi ya kuendelea kudumaa miaka nenda rudi.

Demokrasia duni inatokana na uongozi dhaifu (weak leadership) na mifumo legelege ambayo imegharimu mengi katika Bara la Afrika. 

Pengine ni kutokana na udhaifu huo viongozi wa Afrika walikutana tena nchini Senegal ili pamoja na mambo mengine kujadili namna ya kuimarisha demokrasia.

Akizungumza kuhusu demokrasia, aliyewahi kuwa Rais wa Nigeria, Olusegun Obasanjo aliwataka watawala kuandaa mazingira ya upatikanaji wa demokrasia.

Anachosema Obasanjo ni kuwa watawala wa Afrika wamechezea mno demokrasia na sasa ni muda muafaka wa kuhakikisha tunairejesha (to retrieve).

Obasanjo anasema ni muhimu kufanya hivyo kwa ustawi wa vijana wa sasa na vizazi vijavyo, ingawa alisema demokrasia ina hatua.

Bila kumumunya maneno ni lazima tukiri kuwa viongozi wetu wanatakiwa kubadilika. Kama kweli ni wafuasi wa demokrasia yanayotokea leo Afrika tusingeyaona.

Kwa mfano, angalia namna ulafi wa madaraka unavyosababisha viongozi wetu wachezee katiba za nchi wanavyotaka kana kwamba ni nguo zao. 

Tuwaelewe vipi wanapobadilisha katiba ili tu wasalie madarakani badala ya kuheshimu zilizopo? Ni lipi jema la kuiga kutoka kwa viongozi wa aina hiyo?

Kinachosikitisha ni kuwa kadiri siku zinavyosogea ndivyo viongozi wetu wa zama hizi za utandawazi wanavyochezea katiba na kimsingi hawajali. 

Tuseme imetosha. Afrika inahitaji demokrasia ya kweli ili kuharakisha maendeleo ya nchi zilizopo katika bara hilo na si vinginevyo kwani wamechoka na umaskini.

Wananchi wa bara hilo wana kiu ya kuona haki za binadamu zinaheshimiwa. Nje na hapo viongozi wanaotundika demokrasia msalabani hawatufai.






Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger