KAMPUNI ya
Simu za Mkononi ya Halotel imetoa msaada wa vyakula, mbuzi na mafuta ya
kupikia kwa vituo 10 vya Watoto Yatima na wanaoishi katika mazingira
magumu jijini Dar es Salaam, ikiwa ni mkono wa Siku Kuu ya Eid Mubarak.
Akikabidhi zawadi hizo Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Halotel, Nguyan
Thanh Binh alisema msaada huo ni utaratibu wa kawaida wa kampuni hiyo
kuikumbuka jamii hasa watoto waliopo katika mazingira magumu.
Alisema
mbali na kampuni hiyo kutoa msaada huo kwa watoto yatima na wanaoishi
katika mazingira magumu Dar es Salaam, wamezielekeza ofisi zao mikoa
mbalimbali Tanzania kusaidia makundi hayo kama walivyofanya jijini Dar
es Salaam.
Alisema utaratibu huo utakuwa wa kila mara ili kujenga
mahusiano mazuri na jamii hiyo ambayo pia ni wateja wa kampuni yao.
"...Kwanza
tumeanza kuwaita na kuzungumza nao kujua masuala mbalimbali
yanayowakabili na huu utakuwa ni utaratibu wa kawaida kabisa kujumuika
na makundi haya na kusaidiana," alisema Nguyan Thanh Binh akizungumza na
wanahabari mara baada ya kukabidhi msaada huo kwa vikundi.
Kila
kikundi kimepewa mfuko wa mchele, galoni la mafuta ya kula pamoja na
mbuzi wawili ikiwa ni mkono wa Siku Kuu ya Eid Mubarak inayotarajia
kuadhimishwa kesho duniani pote.
- Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Halotel, Nguyan Thanh Binh (wa pili kushoto) na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa Kampuni ya Halotel, Mhina Semwenda (mwenye kanzu) wakikabidhi kiroba cha mchele, mafuta pamoja na mbuzi wawili kwa baadhi ya viongozi na watoto wa Kituo cha Yatima cha Mwandaliwa cha jijini Dar es Salaam ikiwa ni zawadi ya Eid Mubarak.
SHARE
No comments:
Post a Comment