National Arts Council BASATA
Baraza la
Sanaa la Taifa (BASATA) kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa
linalojishughulisha na Elimu na Sayansi (UNESCO) litaungana na wasanii
mbalimbali nchini na wadau wa Sanaa kuazimisha siku ya muziki wa Jazz
duniani ambayo kwa mara ya kwanza itaazimishwa nchini Mei 2, 2016.
Maazimisho
hayo ambayo yatapambwa na burudani mbalimbali kutoka kwa Wasanii wa
muziki wa jazz hususan Band maarufu ya Das Jazz yanatarajiwa kufanyika
kwenye Ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ofisi za BASATA Ilala Sharif Shamba
jijini Dar es Salaam.
Sambamba
na burudani hizo, kutakuwa na mada mbalimbali zitakazowasilishwa na
wadau wa muziki huu wa jazz ambazo zitalenga kuamsha ari, thamani na
ufahamu wa muziki huu maarufu duniani miongoni mwa wasanii nchini.
Wawasilishaji
wa mada hizo pamoja na mada zao kwenye mabano ni pamoja na John Kitime
(Matumizi ya neno Jazz), Carola Kinasha (Uhusiano kati ya Elimu ya
Muziki na Jazz) na Kurwigira Mareges (Historia ya Muziki wa Jazz) na
Masoud Masoud (Ujue Muziki wa Jazz)
Mbali na
burudani na mada hizo kuhusu muziki huo wa Jazz kutakuwa na wageni
waalikwa kutoka kwenye balozi na vituo vya Utamaduni vya nchi mbalimbali
zilizopo hapa Tanzania
BASATA
linatoa wito kwa wasanii na wadau wa muziki huu wa jazz kujitokeza kwa
wingi katika maadhimisho haya ambayo yatakuwa yakifanyika kila mwaka
sambamba na mataifa mengine duniani.
Sanaa ni kazi, tuipende na kuithamini
Godfrey Mngereza
Katibu Mtendaji – BASATA (P.T)
SHARE
No comments:
Post a Comment