TRA

TRA

Thursday, July 7, 2016

Simulizi Za Kusisimua.. General Idd Amin; Mke Wake Kipenzi, Mtoto Wake Kipenzi..

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !



Ndugu zangu,
Tumeona, kuwa Idi Amin ameishi kwa anasa na mashaka makubwa. Amin hakumuamini mtu yeyote. Nguvu yake kubwa ilikuwa kwenye jeshi na askari kanzu. Wengi wa askari wake walitoka kabila lake la Kakwa na Wanubi wa Sudan.
Idd Amin aliongea lugha kadhaa lakini hakuna lugha aliyoimudu barabara isipokuwa lugha ya kabila lake la Kakwa. Aliongea Kiswahili , cha tabu kidogo. Aliongea Kiingereza, cha tabu kidogo. Kiarabu alijua kidogo pia. Kiganda hivyo hivyo.
Alipokuwa akihutubia hakuonyesha kuwa anakaribia kumaliza hotuba yake. Mara nyingi alimaliza hotuba huku watu wakidhani anaendelea.
Inasemwa, kuwa alifanya hivyo kwa sababu za kiusalama. Idd Amin alijua wengi hawakujua lugha yake ya Kikakwa. Kwa vile walinzi wake wa karibu ni wa kabila lake, basi, alipokaribia kumaliza hotuba yake aliingiza maneno ya lugha ya kabila lake ili kuwaandaa walinzi wake mara atakaposimama ghafla na kuondoka ukumbini.
Kikosi chake cha makachero kilikuwa kinahofiwa sana. Vilikuwa vikosi viwili; Public Safety Unit ( Usalama wa Taifa) na State Research Bureau. Hicho cha mwisho ndio kilikuwa kiboko ya vyote.
Kiliundwa na mabayaye kutoka kabila la Idd Amin. Vijana waliokuwa na elimu ya chini na wengi aliwatoa mitaani. Ndani ya kikosi hicho kulikuwa pia na watu kutoka makabila ya Lugbara ( kabila la mama yake Amin) Madi na Wanubi wa Sudan.
Makachero hao walikuwa na mazoea ya kuvaa mashati ya vitenge. Enzi hizo Uganda, jirani yako akikuambia kuwa umefuatwa nyumbani na watu wanaovaa 'Chitenge', na wakakukosa, basi, cha kufanya si kuwasubiri warudi tena. Unachotakiwa ni kuchukua kinachochukulika na kuutafuta mpaka wa nchi jirani ya karibu na ulipo.
Jamaa hao wavaa ' Chitenge' walitisha sana. Inasemwa, kuwa kila mmoja katika kikosi hicho alikuwa na mawasiliano ya moja kwa moja na Idd Amin. Katikati ya Jiji la Kampala walikuwa na ofisi zao. Ni katika majengo kadhaa. Yalitumika pia kama vituo vya kuwatesa wapinzani au waliodhaniwa wangekuwa wapinzani wa Idd Amin. Ilitokea mtu akapita mitaa ya Kampala na kusikia sauti za watu wanaolia kwa kuteswa. Ilikuwa ni mambo ya kawaida.
Wengi waliteswa hadi kufa. Mara nyingi walitupwa Ziwa Victoria na kuachwa wakiliwa na samaki. Kuna simulizi za wakazi wa kando ya ziwa kuamka na kukuta lori likiwa na walichodhani ni samaki wakubwa. Watu walikimbilia kuwahi kununua samaki hao. Walishangaa kuona ni miili ya binadamu iliyopelekwa kutupwa ziwani.
Pamoja na yote hayo, Idd Amin alikuwa mume wa wake wanne. Alikuwa na mabibi wa pembeni pia. Inasadikiwa, kuwa idadi ya watoto wa Idd Amin ilifikia hamsini!
Katika watoto wote wa Amin , inasemwa kuwa, Idd Amin alimpenda sana Moses ( Pichani). Na katika wake zake wote, alipempenda sana Nadina ( Pichani)
Mara nyingi Amin alionekana akiwa na mtoto Moses. Alimpenda kiasi katika umri mdogo kumvalisha magwanda ya jeshi. Moses alianza kushika bastola katika umri mdogo pia. Hivyo hivyo mkewe Nadina, Idd Amin alimpenda sana Nadina. Amin alionekana mara kwa mara akiwa na Nadina kando yake.
Naam. Simulizi juu ya Idi Amin ni nyingi. Tukijaaliwa, kesho tutachambua ukweli juu ya madai kuwa Idd Amin alimwua mwanawe kipenzi Moses kwa sababu za kishirikina . Inasemwa pia, kuwa aliwahi kumwua mmoja wa wake zake kwa sababu za kishirikina. Je, kuna ukweli katika hayo? Nitakusimulia..
Maggid,
Iringa.(P.T)

Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger