TRA

TRA

Friday, August 26, 2016

Mjamzito akipoteza maisha nani anajali?

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !






Mjamzito akipoteza
maisha nani anajali? 

Julian Msacky

MJAMZITO mmoja akipoteza maisha au mtoto wake wakati wa kujifungua ni watu wachache wanaonekana kujali au kuguswa na kilichotokea. Watu wengi huona tukio hilo la kawaida. 

Ndiyo maana huwezi kusikia serikali ikipiga kelele linapotokea tukio la aina hiyo na hata ikifanya hivyo inakuwa ni mara chache. Si hivyo tu, hata wauguzi hawaoneshi kusononeshwa. Ni business as usual!.

Hii ni hatua mbaya. Ni lazima viongozi waoneshe kuguswa pale taifa linapopoteza raia wake kwa sababu zinazozuilika. 

Ni lazima tujenge utamaduni huo kwani uhai wa mtu una thamani kubwa. Uhai wa mtu haununuliwi, hivyo ni vizuri Serikali kuhakikisha imeweka mfumo mzuri wa kumhudumia mjamzito. 

Tuhakikishe hospitali, zahanati na vituo vya afya vina wahudumu bora.Wahudumu wenye vitendea kazi vya kutosha. 
 Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu (katikati) akimfariji mtoto mchanga

Wahudumu wanaolipwa maslahi mazuri ili waweze kuwahudumia wagonjwa na wajawazito.
Tuhakikishe hakuna mjamzito anayepoteza maisha.Tuhakikishe mjamzito akifikishwa hospitalini anahudumiwa kwa ukaribu. 

Anahudumiwa kwa lugha laini badala ya kutumia kejeli na maneno mengine ya kuzidi kumtia uchungu mjamzito. Ndiyo.

Nchi zilizoendelea ni nadra mjamzito kupoteza maisha wakati wa kujifungua. Ni nadra mtoto kupoteza maisha wakati wa kuzaliwa. 

Kama nchi hizo zimeweza, kwa nini sisi kama nchi tushindwe? Ni lazima tufanye kazi ya ziada ya kumlinda mama mjamzito. 

Haiwezekani nchi kama yetu hadi leo tuendelee kupoteza maisha ya mama na mtoto wakati wa kujifungua. Haiwezekani.

Kama tuna fedha za kujenga barabara, majumba marefu yanayokaribia kugusa angani, ni kwa nini tushindwe kujenga hospitali nzuri kila wilaya na zahanati bora kila kijiji au kata.

Kama tuna madini ya kila aina na yanachimbwa usiku na mchana ni kwa nini tushindwe kumhudumia mama mjamzito ili aweze kuleta kiumbe kipya dunia bila matatizo. Inawezekana. Tujipange.

Leo hii tunaambiwa nchi ina hazina kubwa ya gesi. Ina hazina kubwa ya madini ya heliamu na mengine mengi. Ni kweli tumeshindwa kutumia utajiri huo kuweka mazingira bora ya huduma za afya?

Kwa utajiri uliopo nchini tulitakiwa tuwe na huduma nzuri za afya na wahudumu wenye weledi ili kuokoa maisha ya ndugu na jamaa zetu ambao wanapoteza maisha kwa sababu zinazoepukika. 

Mbali na huduma za afya hususan kwa wajawazito, hatuoni sababu ya watoto wadogo kuendelea kuteseka kwa kukosa huduma muhimu katika maisha yao hata kama wazazi wao hawapo.

Sisi kama nchi ni lazima tuweke mfumo mzuri wa kulinda maisha ya watoto. Wale tunaoimba kila siku ni watoto wa mitaani tukiwawekea mazingira rafiki wataondoka tu mitaani. 

Ni suala la kujipanga. Kwa mfano, tukiwawekea vituo pamoja na wasimamizi wa kuhakikisha wanawatunza na kuhakikisha wanapata elimu, hivi hatutakuwa tumeondoa au kupunguza tatizo?

Kipi bora kuwaacha wanarandaranda mitaani au kuweka mfumo wa kuondoa tatizo. Pamoja na mikakati ya aina hiyo kuna umuhimu wa kila mzazi kutimiza jukumu lake.

Hii ikiwa na maana kuwa tusikwepe majukumu ambayo tumeyataka wenyewe. Katika hili wanawake na wanaume wanaozurura na watoto wakiomba huku wakiwa na nguvu za kufanya kazi, tusiwachekee.

Kama Rais John Magufuli anasema Hapa Kazi Tu ni lazima watu wa aina hiyo wafanye kazi. Kama wenye ulemavu wanafanya kazi za kujipatia riziki sembuse hao wenye nguvu zao!

Wakati tukitafakari hayo, tukumbuke pia kwamba Shirika la Watoto la Umoja wa Mataifa (UNICEF), limetoa ripoti ambayo viongozi wetu ni lazima wakune vichwa na kuangalia namna ya kuwanusuru.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo watoto walio na umri chini ya miaka mitano watafariki kutokana na sababu zinazozuilika kati ya sasa na mwaka 2030.

Katika ripoti yake ya mwaka UNICEF imesema kwamba kulingana na mwenendo wa hivi karibuni na makadirio ya ukuaji wa watu, watoto milioni 167 wataishi katika umaskini uliokithiri.

Si hivyo tu, bali watoto milioni 60 hawataweza kuhudhuria elimu ya msingi na wanawake milioni 750 watakuwa katika ndoa kama watoto ifikapo mwaka 2030.

Hii ina maana gani? Ina maana kuwa suala la usawa lisiposhughulikiwa na nchi kuboresha afya na elimu kuna hatari ya kupoteza viumbe hao. 

Ripoti hiyo ilisema asilimia 80 ya vifo vinavyozuilika vinatokea katika maeneo ya kusini mwa Asia na Jangwa la Sahara ambako ndiko iliko Tanzania.






















 


Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger