TRA

TRA

Sunday, May 28, 2017

Tumesimika mtambo wa uporaji

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !



Julian Msacky

MWANDISHI Tonn Burgis alipoandika katika kitabu chake cha “The Looting Machine” ama mtambo wa uporaji rasilimali za Afrika hakukosea.

Kwa mujibu wa Burgis anashangaa ni kwa nini Afrika inazidi kuwa fukara wakati ina utajiri wa kila aina.

“Ni kwa nini bara hili ni maskini wakati limesheheni utajiri wa kina aina,”alihoji Burgis katika kitabu hicho.

Anachozungumzia mwandishi huyo ni tatizo ambalo lipo nchi zetu za Afrika, ikiwemo Tanzania.

Niharakishe kusema hapa kuwa umakini mdogo wa viongozi wetu ndiyo umesababisha Afrika iwe ilivyo.

   Wanyama aina ya swala

Hii ni kwa sababu baadhi yao wamesimika “mtambo wa uporaji” na kuacha watu pamoja na nchi zao zikiwa taaban.

Mtambo huo wa uporaji unafyonza kila kitu iwe kwa mikataba ya kitapeli ili mradi tu mali zivunwe kama hazina wenyewe.

Angalia namna madini yetu yanavyonunwa kiholela kwa sababu ya kusimika mtambo wa uporaji ili wachache waishi vizuri.

Haikutarajiwa kuona nchi kama yetu tukilia umaskini kwa sababu Mungu ameibariki na kuipa kila kitu.

Swali ni je, neema hiyo nani ananufaika nayo? Je, tulistahili kuwa maskini au tumetengenezewa umaskini?

Kwa nchi yenye almas, dhahabu, shaba na mengine mengi hivi tuna sababu ya kusema nchi ni maskini?

Hivi tatizo ni umaskini kweli au ipo ajenda nyingine chini ya mtambo wa uporaji anaosema mwandishi huyo?

Ni kwa nini tuwe hivyo wakati nchi kama Libya iliweza kutumia mafuta yake na kujitosheleza kwa kila kitu?

Tuliona namna Muammar Gaddafi alivyofanya nchi yake iwe kama peponi na wananchi wake walineemeka mno.

Ameuawa kwa kulinda rasilimali za nchi yake na leo hii Libya imekuwa magofu na uwanja wa mapambano kila kukicha.

Wananchi walirubuniwa na kumchukia kiongozi ambaye aliwafanya waishi kwa furaha na bila ombaomba.

Leo hii Libya haikabiliki. Leo hii Libya haifai. Mataifa ya magharibi yamesimika mtambo wa uporaji na hakika wanavuna. 

Swali hapa ni je, Tanzania tuna kila kitu lakini tumeshindwa kuifanya ionekane kama nchi tajiri. Tumlaumu nani?

Tukisema wananchi ni kukosea. Viongozi wana kila sababu ya kutuambia kwa nini maliasili zetu zimeshindwa kutuneemesha.

Nilitamani kuona madini kama tanzanite ambayo hayapatikani kokote duniani yawe mhimili imara wa uchumi wetu.

Hili limeshindikana. Tanzanite inaendelea kuvunwa na baada ya miaka michache tubakia na mahandaki.

Kama tungetumia vizuri utajiri uliopo nchini leo hii Tanzania ingekuwa nchi ya viwanda zamani za kale.

Lakini kwa vile tumesimika mtambo wa uporaji, mali zinaendelea kumalizika na hatuna viwanda vyovyote vya kujivunia.

Matokeo yake tunakuwa nchi ya kuombaomba hata kwa mataifa ambayo hayana rasilimali kama zetu.

Huo ndiyo ukweli hata kama baadhi yetu hatutaki kusikia. Yanayosemwa kuhusu sekta ya madini wala haishangazi.

Kinachotakiwa kwa sasa ni kuweka mifumo vizuri na viongozi kutanguliza uzalendo kwa ustawi wa nchi yetu.

Bila kufanya hivyo kazi anayofanya Rais John Magufuli itaonekana leo, lakini akiondoka mambo yanabaki vilevile.

Ni mifumo pekee itakayotusaidia na kuhakikisha utajiri wetu unavunwa tukijua kuna leo na kesho.

Tukivuna mali zilizopo kana kwamba Tanzania hatakuwa tena na watu itakuwa ni dhambi kubwa. Ni lazima tubadilike.

Ni lazima viongozi waoneshe kuguswa na matatizo ya wananchi kama alivyokuwa Hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Mwalimu alitunza rasilimali tunazochezea leo hii na pengine baadhi yetu hatuna uchungu nazo ndiyo maana zinatapanywa.

Hii ikiwa na maana kuwa hazitumiwi kwa utaratibu. Zinatumiwa kiholela na hata kile kinachopatikana hakisaidia nchi ipasavyo. 

Kwa mfano, tukiulizwa leo hii fedha za dhahabu tunazitumia kwa kazi gani tutakuwa na majibu ya kuridhisha?

Tukiulizwa fedha zinazopatikana sekta ya utalii zinakwenda wapi au zinafanya jambo gani la kuonekana, tuna majibu mazuri?

Au tangu tuanze kuchimba madini ya tanzanite yamefanya nini kwa nchi na watu wake au tunachimba tu ili siku ziende?  

Binafsi ninadhani kuna kila sababu ya kujipanga upya na kuweka mfumo maalumu wa uvunaji wa rasilimali zetu.

Natamani kuona fedha ya tanzanite inatengewa kazi maalumu mathalani kutoa elimu bure wanafunzi wa chuo kikuu.

Fedha ya dhahabu ielekezwe kwa huduma mathalani za afya kwa maana dawa na vifaa tiba vipatikane vizuri hospitalini.

Vivyo hivyo kwa rasilimali nyingine ambazo tumepewa bure na Mungu lakini tunazitumia ndivyo sivyo.

Kwa kufanya hivyo ingesaidia kupunguza mitambo ya uporaji ambayo imefanya nchi na Afrika iwe kama shamba la bibi.  


Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger