TRA

TRA

Thursday, June 8, 2017

Mafundi 12 vipofu wawasaidia nguo wanafunzi vipofu 60 wa Dar es Salaam

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !


Mwandishi Wetu, Dar

Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (Tantrade) imekabidhi nguo wanafunzi wasioona 60 wa Shule ya Msingi Toangoma jijini hapa zilizoshonwa na kikundi cha wasioona kinachosimamiwa na mamlaka hiyo.

Nguo hizo ni msaada ulitolewa na wahitimu  12 wa mafunzo ya ushonaji ili  kuwatia moyo watoto wenye ulemavu na kuwashawishi wasikate tamaa kwa sababu ya maumbile yao.

Akikabidhi nguo hizo hivi majuzi, Ofisa Mawasiliano Mkuu wa Tantrade, Theresa Chilambo alieleza faraja ya mamlaka yao kwa kushuhudia nguo zilizoshonwa na mafundi wasioona zinatumika kwa manufaa katika jamii.





“Sisi katika mamlaka tunafarijika  na kuona fahari  kwa tukio hili.  Lengo letu ni kuwatia moyo watoto wenye ulemavu  kufanya mambo yanayowezekana.  Watafanya mambo hayo kama watawezeshwa na iwapo wataweka juhudi katika jambo wanaloliwania,” alisema Chilambo.

Alieleza kuwa vijana walioshona nguo hizo wanatoa ujumbe kwa vijana wenzao wenye ulemavu  kwamba njia pekee ya kukabiliana na changamoto zinazowakabili ni kukubali hali waliyonayo  na kujituma.

Aliwaomba wadau wa maendeleo na hasa wafanyabiashara kuwasaidia watoto wenye ulemavu wa aina mbali mbali ili wapate elimu itakayowaongoza kufikia malengo waliyojiwekea.

Tantrade inasimamia Programu ya Mafunzo ya ushonaji kwa wasioona yanayoongozwa na Bw.Abdallah Nyangalio ambaye ni kipofu pia na Chilambo amesisitiza: “Tumewahakikishia soko la bidhaa zao kupitia kituo cha huduma ya biashara cha mamlaka hii.”
 
Nyangalio naye amesema kuwa anafarijika kupata watu  wenye juhudi na moyo wa kujifunza na kushona nguo hata kufikia hatua ya kutoa msaada kwa watu wenye mahitaji maalumu katika jamii.  Shule  ya Toangoma imo katika Wilaya ya Temeke. Nyangalio anasimamia mafunzo haya ili kutoa fursa kwa walemavu wengine kupata ujuzi na baadae kujiajiri.

Mafunzo haya yameanza katika Wilaya ya Temeke, baadaye yataendeshwa katika wilaya zote za mkoa wa Dar es Salaam na kisha nchi nzima.

Mwalimu wa kitendo cha wasioona Bibi.Subira Shedangio, amesema kitendo cha  wasioona  kushona nguo na kutoa msaada ni ushahidi  kuwa ulemavu si sababu ya kutofanya maendeleo.

"Kikubwa ni uwezeshaji wa nyenzo na wanafunzi  kuwa na nia ya dhati kwa jambo wanalotaka kufanya. Mawili yakiwepo tunaweza kujiletea maendeleo,”alisema.
Tantrade inaendesha programu hii kuwapa walemavu ujuzi waweze kujitegemea.


Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger