KIKAO CHA BARAZA LA MAWAZIRI LA NCHI ZA
UMOJA WA MASHARIKI NA KUSINI MWA AFRIKA WA UDHIBITI UTAKASISHAJI FEDHA
HARAMU (ESAAMLG).
Baraza la Mawaziri kutoka Umoja wa Nchi za
Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Udhibiti Utakasishaji Fedha Haramu
“The Eastern and Southern Afrika Anti Money Laundering Group – ESAAMLG”,
litakutana Tanzania tarehe 08 Septemba 2017, katika ukumbi wa Hoteli ya
Zanzibar Beach Resort, Visiwani Zanzibar.
Aidha, mkutano huo utatanguliwa na Mkutano
wa Maafisa Waandamizi (Makatibu Wakuu) utakaofanyika kuanzia tarehe 02 –
06 Septemba, 2017 katika ukumbi wa Hoteli hiyo ya Zanzibar Beach
Resort.
DK PHILIP MIPANGO
DK PHILIP MIPANGO
Kwa sasa Tanzania ndio Mwenyekiti wa
Umoja huo kwa kipindi cha mwaka mmoja, baada ya kupokea Uenyekiti kutoka
Jamhuri ya Zimbabwe iliyomaliza muda wake mwezi Agosti, 2017, ambapo
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. PHILIP ISDOR MPANGO (MB), ambae pia
ni Mwenyekiti “President of the Council” ataongoza Mkutano huo.
Katika Mkutano huo, pamoja na masuala
mbali mbali yatakayojadiliwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, itatumia fursa hiyo kuwasilisha Taarifa ya hatua iliyofikia
katika utekelezaji wa Mpango wa “Financial Action Task Force” (FATF)
ulioasisiwa mwaka 2009.
Mpango huo ulizitaka nchi wanachama
kufanya Tathmini ya utekelezaji wa maazimio yaliyoainishwa kwenye FATF,
katika maeneo mbalimbali ya Kisheria, Kisera, Miongozo ya Kitaasisi
zikiwemo Sekta za Fedha na maeneo ya ushirikiano wa kimataifa. Lengo
ni kubaini jinsi nchi wanachama zilivyojipanga katika kudhibiti suala
la Utakasishaji Fedha Haramu na Ufadhili wa Ugaidi (Anti-money
Laundering and Combating the Financing of Terrorism).
Katika mkutano huo, mbinu na mikakati
mbali mbali itakayosaidia kudhibiti Utakasishaji Fedha Haramu na
Ufadhili wa Ugaidi itajadiliwa, hatua ambayo italeta matokeo chanya na
kuongeza kasi ya ukuaji wa Uchumi na kufikia maendeleo tarajiwa katika
Nchi yetu na nchi wanachama kwa ujumla.
Tanzania ni miongoni mwa Nchi waanzilishi
wa Umoja huo ulioasisiwa jijini Arusha, mwaka 1999, Nchi nyingine ni
Uganda, Kenya, Mauritius, Namibia, Sychelles na Swaziland ambazo
zilisaini makubaliano (Memorandum of Understanding – MOU). Hatua ambayo
ilisababisha Makao Makuu ya Sekretariati ya Umoja huo wenye nchi
wanachama (18) ambazo ni Angola, Botswana, Ethiopia, Kenya, Lesotho,
Madagascar, Malawi, Mauritius, Msumbiji, Namibia, Rwanda, Afrika Kusini,
Swaziland, Sychelles, Tanzania, Uganda, Zambia na Zimbabwe kuwa
jijini Dar es Salaam Tanzania.
IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO.
SHARE
No comments:
Post a Comment