TRA

TRA

Friday, August 11, 2017

YAH: KUANZISHWA KWA MFUKO WA ELIMU YA JUU WA TSSF

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !


TANZANIA SOCIAL SUPPORT FOUNDATION
Ofisi ya Mkurugenzi Mkuu
 MFUKO WA ELIMU YA JUU


 



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
YAH: KUANZISHWA KWA MFUKO WA ELIMU YA JUU WA TSSF
1 Utangulizi

Ndugu Wanahabari,
Tanzania Social Support Foundation inayo heshima kubwa mbele yenu kwanza kumshukuru Mwenyenzi Mungu aliyetujaalia uzima na nguvu za kuweza kufika hapa tulipo, pamoja afya njema, vitu ambavyo vimetufanya leo hii tuweze kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi, kila mmoja kwa nafasi yake katika jamii. 

Pia TSSF inawashukuru sana kwa kuwa mmekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha kuwa mnaihabarisha jamii na hivyo kuutekeleza wajibu wenu vema na kwa ufanisi mkubwa. 

Vilevile TSSF inachukua fursa hii kutoa salamu za pole kwenu kutokana na changamoto mbalimbali ambazo zinaikabili sekta ya habari hapa nchini lakini tunawasihi kwamba mzidi kujiimarisha ili muweze kukabiliana na misukosuko mbalimbali ambayo itakuwa inaathiri shughuli zenu. 

Aidha TSSF inawahakikishia kwamba, ipo pamoja na ninyi na itakuwa tayari kutoa msaada wake kwenu pale itakapo hitajika kufanyika hivyo. 

2.      Mfuko wa Elimu ya Juu wa TSSF
Ndugu Wanahabari,
Tangu kurasimishwa kwa Sera ya Taifa ya Elimu ya Juu ya Mwaka 1999, kumekuwepo na ongezeko la watanzania wengi ambao wana hitaji la kupata elimu ya juu walau kwa ngazi ya stashahada pamoja na shahada ya kwanza. 

Hitaji hili ndilo lililofanya kuanzishwa kwa Sheria ya Vyuo Vikuu, Sura ya 346 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Sura ya 178 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheria ya Mfuko wa Elimu, Sura ya 412 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 

Kutokana na kuanzishwa kwa sheria hizi, tumeona vyuo vikuu vingi vikianzishwa chini ya sheria ya vyuo vikuu ambapo tulikuwa na vyuo vikuu vitatu (03) mwaka 1999 lakini mwaka huu wa 2017 tuna vyuo vikuu (vyuo vikuu, vyuo vikuu vishiriki, vituo na taasisi za vyuo vikuu pamoja na vyuo visivyokuwa vyuo vikuu lakini vinatoa elimu ya juu)  tisini na vinane (98) ambapo vyuo vikuu arobaini na vitano (45) kati ya vyuo vikuu  tisini na vinane (98) vinamilikiwa na serikali na vyuo vikuu hamsini na vinne (54) kati ya vyuo vikuu tisini na vinane (98) vinamilikiwa na sekta binafsi. 
Aidha kwa Mwaka 2016/2017 Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania ilidahili wanafunzi wa elimu ya juu wapatao 69,539 ambapo idadi hiyo ya wanafunzi wa elimu ya juu iliongezeka ikilinganishwa na Mwaka 2015/2016 ambapo wanafunzi waliodahiliwa ni 64,919 na tofauti ya ongezeko la wanafunzi waliodahiliwa katika elimu ya juu kwa takwimu za miaka 2015/2016 na 2016/2017 ni 4,620. 
 
Aidha Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, Sura ya 178 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo bodi hiyo ina jukumu la kutoa mikopo na ruzuku kwa wanafunzi wa elimu ya juu hapa nchini. Katika Mwaka wa Masomo 2016/2017 Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ilipokea maombi 88,163 ambapo waliopata mikopo  ni wanafunzi 28,785 sawa na 32.7% ya waombaji wote ambao waliomba mkopo wa elimu kutoka bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu. Vilevile waombaji waliokosa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ni 59,378 sawa na 67.3% ya waombaji wote ambao waliomba mkopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu.
Kwa upande mwingine, Mfuko wa Elimu ambao umeanzishwa chini ya sheria ya Mfuko wa Elimu, Sura ya 412 ya Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umekuwa ukihamasisha uchangiaji ili kuongeza nguvu za Serikali katika kugharamia miradi ya elimu. Miradi ya Mfuko wa Elimu ambao unasimamiwa na Mamlaka ya Elimu Tanzania imekuwa ikijikita katika kuimarisha miundombinu ya taasisi za elimu ambazo zinamilikiwa na serikali na zile zinazomilikiwa na sekta binafsi.
Hivi karibuni, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania ilitangaza kwamba, haitodahili wanafunzi wa elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2017/2018  kupitia mfumo wa udahili wa pamoja ambao unafahamika kitaalam kama “Central Admission System” badala yake wanafunzi wanapaswa kuomba nafasi za kujiunga na chuo kwenye chuo husika moja kwa moja. Utaratibu huu mpya wa udahili ambao ulikuwepo kipindi cha nyuma kabla ya mwaka 2010 umeleta ushindani mkubwa kwa vyuo vikuu hasa vyuo binafsi kutokana na ukweli kwamba, vyuo vikuu ambavyo vinamilikiwa na sekta binafsi hutegemea zaidi mapato yanayotokana na ada ili viweze kujiendesha ikitofautishwa na vyuo vikuu ambavyo vinamilikiwa na serikali ambavyo hupokea ruzuku kutoka serikalini kwa ajili ya kujiendesha, sanjari na watumishi wake kulipwa mishahara yao na serikali.
Kutokana na changamoto hiyo, vyuo vikuu vingi hasa vinavyomilikiwa na sekta binafsi vipo hatarini kufa au kufungwa kutokana na sababu kwamba vipo vyuo vikuu maarufu ambavyo vitajizolea wanafunzi wengi kutokana na umaarufu wake, na vile vyuo vikuu ambavyo ni vichanga vitapata wanafunzi wachache sana na hivyo kupelekea kushindwa kujiendesha. Siyo kwamba vyuo vilivyopo hapa nchini vimekuwa vingi sana la hasha! bali uhitaji wa watanzania ambao wanataka kupata elimu ya juu ni mkubwa hasa unapolinganisha takwimu za wanafunzi wanaodahiliwa kwenye vyuo vikuu dhidi ya takwimu za wale ambao wanaomba mikopo kutoka bodi ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu kama zilivyokwisha kufafanuliwa hivi punde.
Sanjari na hilo, hali ya kiuchumi ya watanzania walio wengi inafahamika kuwa ni masikini ambao hawawezi kugharamia elimu ya juu na kwamba; chanzo maarufu cha kufadhili masomo ya shahada ya kwanza kwa wanafunzi wa elimu ya juu wanaosoma hapa nchini ni kimoja na ni Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ambapo Bodi hiyo kwa sasa imezidiwa na maombi ya wanaotaka mikopo hiyo kutokana na ukomo wa bajeti yake jambo ambalo limeisababisha TSSF kufikiri namna ya kuwasaidia watanzania wanaotamani kujiunga na masomo ya shahada ya kwanza ilhali wamekosa ufadhili kutoka bodi ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu pamoja na vyanzo vingine vya ufadhili.
Ni katika fikra hizo ambapo TSSF kwa kushirikiana na mfadhili wake anayeitwa CDF International kutoka Seattle, Washington, Nchini Marekani imeanzisha Mfuko wa Elimu ya Juu wa TSSF ambao utakuwa ukitoa ufadhili wa masomo ya shahada ya kwanza kwa wanafunzi wa elimu ya juu ambao hawana uwezo wa kujisomesha chuo kikuu na wamekosa ufadhili wa masomo ya shahada ya kwanza kutoka bodi ya mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu pamoja na vyanzo vingine vya ufadhili wa masomo ya shahada ya kwanza.
Wanafunzi watakaofadhiliwa na Mfuko wa Elimu ya Juu wa TSSF ni wale ambao wanasoma kwenye vyuo vikuu vilivyopo ndani ya mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tu. Kwa Mwaka huu wa 2017, TSSF kupitia mfuko wake wa elimu ya juu imeshatangaza kupokea maombi ya ufadhili kupitia tovuti yake ya https://tssf-org-tz.weebly.com/news.html vilevile taarifa ya kupokea maombi hayo imeshatumwa kwa vyuo vikuu vyote nchini.
Mwanzoni mwa Mwaka 2018 TSSF itafanya warsha kubwa  ya vyuo vikuu nchini kwa ajili ya kuanzisha mpango wa msaada wa ufadhili wa masomo vyuoni (Financial Aid Programme) ambapo mpango huo utafadhiliwa na Mfuko wa Elimu ya Juu wa TSSF ili kuhakikisha kwamba Mtanzania hakosi fursa ya kujiunga na elimu ya juu kwa sababu ya kushindwa kujilipia. Mpango huo utakuwa ni kwa vyuo vikuu vyote nchini na kila chuo kikuu kitakuwa na afisa wa dawati la kushughulikia mpango huo. Mpango wa ufadhili wa masomo ya chuo kikuu ni mpya kwa hapa Tanzania lakini umezoeleka katika vyuo vikuu vilivyopo nchini Marekani, Canada, Uingereza pamoja na nchi za bara la Ulaya. Ni imani ya TSSF kwamba, kupitia mpango huu TSSF italeta mapinduzi makubwa na kutoa mchango wake katika kufadhili na kuwezesha elimu ya juu hapa Tanzania.
TSSF inawaomba watanzania wote, wanafunzi wa elimu ya juu, na taasisi za elimu ya juu kushirikiana kwa pamoja katika kufanikisha mpango huu ili vijana wetu wa kitanzania waweze kuwezeshwa kupata elimu ya juu yenye tija, maarifa, na ujuzi utakaowawezesha kumudu maisha yao na hatimaye kuharakisha michakato ya upatikanaji wa maendeleo katika nchi yetu.
Aidha tunawaomba ninyi ndugu wahariri wa vyombo vya habari pamoja wanataaluma wote wa habari kuipa uzito taarifa hii na kutupa ushirikiano wa dhati ili vijana wetu waweze kujiunga na kupata elimu ya juu hapa nchini. Tukumbuke kwamba ngao ya taifa lolote ambalo limeendelea ni elimu bora iletayo maarifa na ujuzi wa kujitambua na kumiliki mazingira ipasavyo na hivyo sisi TSSF tupo kwa ajili ya kuwawezesha vijana wetu wa kitanzania kiuchumi ili waweze kuipata elimu hiyo itakayowawezesha kujitambua na kumiliki mazingira yao ipasavyo na hatimaye tuweze kufikia malengo yetu ya kuwa Taifa la Uchumi wa Viwanda.

Asanteni kwa kunisikiliza!

Imetolewa na


Donati Salla
MKURUGENZI MKUU



           



Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger