Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Phillip Mpango
HOTUBA YA WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO, MHESHIMIWA DKT. PHILIP
I. MPANGO (MB), AKIWASILISHA BUNGENI MAPENDEKEZO YA SERIKALI
KUHUSUMAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2016/2017
TANGULIZI
1. Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lipokee, lijadili na
kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha
2016/17. Pamoja na hotuba hii, ninawasilisha vitabu vinne vinavyoelezea
kwa kina makadirio ya Bajeti. Kitabu cha Kwanza ni Makadirio ya Mapato;
Kitabu cha Pili ni Makadirio ya Matumizi ya Kawaida kwa Wizara, Idara
za Serikali zinazojitegemea, Taasisi na Wakala za Serikali; Kitabu
cha Tatu ni Makadirio ya Matumizi ya Kawaida kwa Mikoa na Mamlaka za
Serikali za Mitaa; na Kitabu cha Nne ni Makadirio ya Matumizi ya
Maendeleo kwa Wizara, Idara za Serikali zinazojitegemea, Taasisi na
Wakala za Serikali, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za
Mitaa. Aidha, upo Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka 2016 pamoja na
Muswada wa Sheria ya kuidhinisha matumizi ya Serikali wa mwaka 2016
ambayo ni sehemu ya Bajeti hii.
2. Mheshimiwa
Spika, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mungu kwa baraka na amani
anayoendelea kuijalia nchi yetu na pia kwa kuniruhusu kusimama hapa
mbele ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwasilisha Bajeti ya
Serikali kwa mwaka 2016/17. Aidha, kwa namna ya pekee nachukua fursa hii
kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuchaguliwa
kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Samia Suluhu
Hassan kuwa Makamu wa Rais na mwanamama wa kwanza kushika nafasi hiyo
katika historia ya nchi yetu. Nampongeza pia Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed
Shein, kwa kuchaguliwa tena kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar. Vilevile, nampongeza Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa kwa
kuchaguliwa na wananchi wa jimbo la Ruangwa kuwa Mbunge wao na kuteuliwa
na Mhe. Rais na kuthibitishwa na Bunge kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania. Napenda pia kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika
pamoja na Naibu Spika kwa kuchaguliwa kuongoza Bunge letu
Tukufu. Kadhalika, natumia fursa hii kumpongeza Mhe. Mohamed Othman
Chande, Jaji Mkuu wa Tanzania, kwa kuongoza mhimili wa Mahakama kwa
weledi mkubwa.
3. Mheshimiwa
Spika, niruhusu pia niwashukuru sana waheshimiwa wenza wa viongozi wetu
wa kitaifa: Mama Janet Magufuli, Bwana Ameir Hafidh Ameir (mume wa Mhe.
Makamu wa Rais), Mama Mwanamwema Shein, Mama Mary Majaliwa, Mama Fatuma
Ramadhani Mganga (mke wa Mhe. Spika), Bwana James Andilile (mume wa
Mhe. Naibu Spika) na Mama Saada El-Maamry Othman (mke wa Mhe. Jaji Mkuu)
kwa kuwasaidia na kuwatunza viongozi wetu vizuri. Asante kwenu wote na
Mungu awabariki.
4. Mheshimiwa
Spika, kwa mara nyingine natoa shukrani za pekee kwa Mhe. Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
kuniteua kuwa Mbunge na Waziri wa Fedha na Mipango. Ninatambua kwamba
wananchi wa Tanzania wananidai! Tarehe 29 Februari, 1968 Baba wa Taifa
hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwasilisha hati ya madai kama
ifuatavyo, nanukuu: “Tunadai nini basi kwa wale wenzetu waliojaliwa
kupata elimu? Tunadai huduma kwa wananchi na huduma ambayo ukubwa wake
utalingana na kiasi cha elimu waliyoipata” mwisho wa kunukuu. Hivyo,
napenda kumuahidi tena Mhe. Rais na Watanzania kwamba nitaibeba dhamana
hii kwa bidii na uadilifu ili kulipa deni langu kwa nchi yangu.
Vilevile, nawapongeza waheshimiwa Wabunge wote kwa kuchaguliwa kwenu na
kuwa sehemu ya Bunge hili. Napenda pia kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri
wenzangu na Naibu Mawaziri kwa dhamana kubwa tuliyopewa na Mheshimiwa
Rais kuwatumikia Watanzania. Nampongeza pia Dkt. Thomas Kashililah,
Katibu wa Bunge na Bw. Hussein Kattanga, Mtendaji Mkuu wa Mahakama kwa
kuratibu vyema shughuli za Bunge na Mahakama kwa mtiririko huo. Napenda
pia kumpongeza Prof. Mussa Assad, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za
Serikali kwa kazi nzuri anayoifanya ya kukagua na kutoa taarifa za
matumizi ya fedha za umma kwa wakati.
5. Mheshimiwa
Spika, ninaishukuru sana Kamati ya Bunge ya Bajeti chini ya uenyekiti
wake Mhe. Hawa Abdulrahman Ghasia, Mbunge wa Mtwara vijijini na Makamu
Mwenyekiti Mhe. Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kwa
kuchambua kwa kina bajeti za Mafungu yote na kutoa mapendekezo na
ushauri. Aidha, napenda kuwashukuru wenyeviti wa kamati za kisekta kwa
ushauri na mapendekezo waliyotoa wakati wakichambua rasimu ya Bajeti
hii. Ninamshukuru pia Mhe. George Mcheche Masaju (Mb), Mwanasheria Mkuu
wa Serikali kwa kutayarisha kwa wakati Muswada wa Sheria ya Fedha wa
mwaka 2016 na Muswada wa Sheria ya Matumizi wa mwaka 2016 ambayo ni
sehemu ya Bajeti hii.
6. Mheshimiwa
Spika, napenda kumpongeza Mhe. Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji, Mbunge wa
Jimbo la Kondoa kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango na
pia ninamshukuru kwa ushirikiano anaonipatia katika utekelezaji wa
majukumu yangu. Aidha, napenda kumshukuru Dkt. Servacius B. Likwelile,
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha na Mipango kwa uratibu na usimamizi mzuri
wa maandalizi ya Bajeti hii. Kadhalika, nawashukuru Naibu Makatibu
Wakuu; Gavana wa Benki Kuu; Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania;
Msajili wa Hazina; Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu; Wakuu
wa taasisi zilizo chini ya Wizara; Wakuu wa idara, vitengo na Watumishi
wote wa Wizara na taasisi zake kwa kazi kubwa waliyoifanya kukamilisha
Bajeti hii.
7. Mheshimiwa Spika, Bajeti
hii imezingatia mawazo na mapendekezo ya wadau mbali mbali wakiwemo
wenye viwanda, wafanyabiashara na wengine wengi. Nawashukuru wote kwa
mawazo na ushauri wao. Kipekee niwashukuru wajumbe wa kamati ya
wataalamu na ushauri wa masuala ya kodi (Task Force) na kamati ya
kitaifa ya ushauri wa kodi (Think Tank) kwa ushauri wao mzuri walionipa.
8. Mheshimiwa Spika,kwa
kukamilisha shukrani hizi, napenda kutoa shukrani maalum kwanza kwa
Prof. Benno Ndulu, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, mwalimu wangu na
mfano bora wa maisha yangu kikazi. Amenilea kitaaluma na kikazi tangu
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Benki ya Dunia, na ameendelea kunishauri
katika utumishi wangu Serikalini. Ninamshukuru sana kwa uzalendo na
unyenyekevu wake na ninamtakia kheri na afya njema yeye na familia yake.
Pia ninapenda kutoa shukrani maalum kwa rafiki yangu mpenzi, mke wangu
Mbonimpaye kwa kunitunza vizuri, lakini hasa kwa kuniombea msaada wa
Mungu siku zote akishirikiana na watoto wetu, wanafamilia wengine na
marafiki zetu. Asanteni na Amani iwe kwenu! Aidha nawashukuru viongozi
wa dini mbalimbali na watanzania wote ambao waliitikia rai ya Rais wetu
Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kumuombea na wanatuombea sana na
sisi wasaidizi wake ili tujitoe na kuwatumikia watanzania, na hasa
maskini, kwa bidii na unyenyekevu. Mungu awabariki! Kadhalika,
nawashukuru sana wananchi wa kijiji cha Kasumo, wilaya ya Buhigwe
nilikozaliwa, pamoja na wananchi wa Kasulu na mkoa wa Kigoma kwa ujumla.
Asanteni kwa kunilea na kwa mapenzi yenu mema.
9. Mheshimiwa
Spika, hotuba hii inawasilisha Bajeti ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya
Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yenye kauli mbiu ya “Hapa Kazi Tu”.
Serikali inaleta Bajeti hii kwa dhamira ya kweli ya kutekeleza ahadi
zake zilizopo katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2015 – 2020, Mpango wa
Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/17-2020/21 na Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2025 ili kukidhi kiu na matarajio ya Watanzania. Malengo makuu
ya kiuchumi ya Bajeti hii ni mawili. Kwanza ni kutatua matatizo
yanayowakabili wananchi ili kuleta matumaini mapya ya maisha mazuri
zaidi kwa wananchi wetu, hasa wa kipato cha chini. Lengo hili
litahusisha kufanya mabadiliko makubwa katika utendaji wa Serikali,
hususan kurejesha nidhamu ya kazi na uwajibikaji, na kuondokana na
ufanyaji kazi kwa mazoea, pia kuimarisha uadilifu na usimamizi wa
matumizi ya mali za umma na rasilimali za Taifa. Pili ni kujenga uchumi
wa kipato cha kati kiuhalisia kwa kusimamia kwa umakini utulivu wa
uchumi na uendelezaji wa viwanda vitakavyoongeza ajira hasa kwa vijana
wetu nchini na kuongeza tija kwenye kilimo ili kuongeza kipato katika
sekta hii inayotegemewa na wananchi wengi.
10. Mheshimiwa
Spika, wakati Mheshimiwa Rais akifungua Bunge hili tarehe 20 Novemba
2015, alibainisha maeneo yanayolalamikiwa sana na wananchi, na kuelekeza
Wizara, Ofisi na Taasisi husika zijipange ipasavyo kutatua malalamiko
hayo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Naomba niyarejee kwa kifupi.
Kwanza ni rushwa katika maeneo yote ya utoaji huduma kwa wananchi; Pili,
ni upotevu wa mapato, ujangili, wizi, ubadhirifu, matumizi mabaya ya
fedha, uzembe na urasimu katika maeneo mbalimbali; eneo la tatu ni
huduma zisizoridhisha za upatikanaji wa maji, elimu bora na afya; eneo
la nne ni migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, vijiji na
hifadhi, wananchi na wawekezaji, wananchi na wamiliki wa mashamba pori
na uvunjaji wa sheria za ardhi.
11. Mheshimiwa
Spika, eneo la tano ni huduma zisizoridhisha za usafiri na usafirishaji
kutokana na uchakavu wa miundombinu ya reli, barabara, usafiri wa
majini; na udhaifu mkubwa wa shirika la ndege. Eneo la sita ni upungufu
katika utoaji haki ikiwa ni pamoja na mlundikano wa kesi mahakamani,
wananchi kubambikiwa kesi na polisi, makazi duni na ukosefu wa vitendea
kazi kwa askari; eneo la saba ni kodi na tozo za kero kwenye mazao,
uhaba wa zana na pembejeo za kilimo, mifugo na uvuvi, uhaba wa masoko ya
uhakika, maghala, maafisa ugani na huduma za ugani, na uvuvi haramu; na
eneo la nane ni uwezeshaji mdogo kwa makundi maalum hususan wazee,
walemavu, wanawake, watoto, vijana, wafanyakazi, wasanii, wanamichezo,
wachimbaji wadogo na watumishi wa vyombo vya ulinzi na usalama.
12. Mheshimiwa
Spika, baada ya rejea hiyo, naomba niseme tena kwamba mkazo mkuu wa
Bajeti hii ni kutekeleza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kutatua
kero za wananchi. Aidha, Serikali itatekeleza azma ya kuendeleza viwanda
ambavyo ndiyo msingi wa uchumi endelevu utakaowezesha Taifa letu
kufikia hadhi ya kipato cha kati na hali bora ya maisha ya wananchi
walio wengi ifikapo mwaka 2025.
13. Mheshimiwa
Spika, Bajeti ya Serikali ya mwaka 2016/17 inalenga kuimarisha
miundombinu ya msingi kama vile ya maji, umeme na usafirishaji kwa ajili
ya kuhakikisha maendeleo ya viwanda nchini na vile vile kuongeza
uzalishaji wa mazao ya kilimo yanayotumika kama malighafi viwandani. Ili
kufanikisha hilo, mkazo mkubwa utawekwa kwenye ukusanyaji wa mapato ya
ndani pamoja na ugawaji wa rasilimali hizo katika maeneo muhimu ya
kuvutia uwekezaji kwenye sekta ya viwanda. Jitihada kubwa zitaelekezwa
katika kuziba mianya ya ukwepaji kodi, kuibua vyanzo vipya vya mapato,
na kuhimiza matumizi ya mashine za kielektroniki - EFDs ili kuongeza
makusanyo na vile vile kudhibiti matumizi yasiyokuwa na tija. Hivyo,
kauli mbiu ya Bajeti za nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki
kwa mwaka 2016/17 ni “kuongeza uzalishaji viwandani ili kupanua fursa za
ajira” (Industrial growth for job creation). Kwa msingi huo, Bajeti ya
maendeleo kwa mwaka 2016/17 imeongezwa kwa kiasi kikubwa na kufikia
asilimia 40 ya bajeti yote tofauti na miaka yote ya nyuma ambapo ilikuwa
wastani wa asilimia 25. Bajeti hii pia inalenga kujenga mazingira
mazuri ya kufanya biashara na kuwekeza ili kuvutia ushiriki wa
wawekezaji wa ndani na nje katika kuendeleza viwanda na kilimo.
I. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA MWAKA 2015/16
14. Mheshimiwa
Spika, mpango na bajeti ya Serikali mwaka 2015/16 ililenga kukusanya
kiasi cha shilingi trilioni 22.49 kutoka kwenye vyanzo vya ndani na nje.
Kati ya kiasi hicho, shilingi trilioni 13.99 zilikuwa ni makadirio ya
mapato ya ndani zikijumuisha mapato ya Halmashauri; shilingi trilioni
2.32 ni mikopo nafuu na misaada kutoka kwa Washirika wa Maendeleo;
shilingi trilioni 4.03 ni mikopo ya kibiashara ya ndani; na shilingi
trilioni 2.14 ni mikopo ya kibiashara ya nje. Aidha, kiasi cha shilingi
trilioni 16.57 kilipangwa kutumika kwenye matumizi ya kawaida na
shilingi trilioni 5.92 kwenye matumizi ya maendeleo.
SHARE








No comments:
Post a Comment