
Mwanajeshi wa Syria akipeperusha bendera ya nchi yake mjini Aleppo.
Waasi wa
Syria wameanzisha operesheni kubwa dhidi ya maeneo yanayodhibitiwa na
serikali kusini magharibi mwa Aleppo, ikiwa ni hatua ya kwanza kubwa
tangu walipopoteza maeneo hayo kwa jeshi.
Kituo cha
kijeshi cha waasi kinachojumuisha kundi jipya lenye itikadi kali la
Jabhat Fatah al Sham, kimetangaza kudhibiti maeneo ya kijeshi ya
serikali Kusini Magharibi mwa mji wa Allepo, katika saa za kwanza za
oparesheni ya kusitisha kuzingirwa kwa maeneo ya waasi na vikosi vya
serikali.
Aidha
serikali ya Syria imethibitisha mashambulizi hayo kupitia kituo cha
habari cha kitaifa lakini ikasema vikosi vyake vimefanikiwa kuwasogeza
waasi kando na kambi ya kijeshi, huku ikikanusha taarifa ya kutekwa
shule ya Hikma na waasi hao.
Bado robo
ya milioni ya raia wanaishi katika maeneo yanayoshikiliwa na upinzani
Mashariki mwa mji wa Allepo, mji uliozingirwa kuanzia jeshi
lililosaidiwa na vikosi vya kijeshi vya Iran lilipoziba barabara ya
kuingia katika miji ya waasi mapema mwezi Julai.
Aleppo,
moja ya miji mikubwa nchini Syria kabla ya kuanza machafuko miaka mitano
iliyopita umegawika kati ya vikosi vya serikali na waasi tangu kipindi
cha kiangazi mwaka wa 2012. Aidha Kuudhibiti tena mji huo itakuwa
ushindi mkubwa kwa serikali ya Rais Bashar al Assad wa Syria tangu Urusi
ilipojiunga na serikali ya Syria katika vita hivyo mwaka uliopita.
Siku ya
Alhamisi, serikali ya Assad na mshirika wake Urusi walitangaza
oparesheni ya pamoja katika eneo lililozingirwa kwa kutoa vijikaratasi
vinavyowataka wapiganaji kusalimu amri na raia kuondoka katika maeneo
hayo.
Hata
hivyo serikali ya Marekani imetilia shaka hatua hiyo na kusema huenda
ikawa ni mipango ya kupunguza idadi ya watu mjini Allepo, eneo muhimu
kwa upinzani nchini humo ili iwe rahisi kwa serikali kuudhibiti tena.
Marekani yatangaza kuchukuwa sehemu kubwa ya Manbij
Huku hayo
yakiarifiwa msemaji wa vikosi vinavyoongozwa na Marekani ametangaza
kuchukua udhibiti wa takriban asilimia 70 ya mji wa Manbij kaskazini mwa
Syria kutoka kwa waasi wa Dola la Kiislamu (IS) baada ya kupiga hatua
muhimu mnamo siku mbili zilizopita.
Jeshi la
Waasi wa Syria wajulikanao kama Syrian Democratic Forces, likishirikiana
na wanamgambo wa kikurdi YPG pamoja na wapiganaji wa kiarabu
walianzisha kampeni miezi miwili iliyopita wakiongozwa na jeshi maalum
la Marekani kupambana na wanamgambo wa IS katika eneo la mpakani mwa
Syria na Uturuki.
Huku raia
2,300 wakiripotiwa kuutoroka mji wa Manbij, maelefu ya wakaazi bado
wamekwama mjini humo. Hata hivyo, kuwepo kwa wakaazi katika mji huo
waliokuwa wanazuwiwa kuondoka na wanamgambo wa IS kulitatiza kwa kiwango
fulani mashambulizi ya angani ya Marekani hii ikiwa kwa mujibu wa duru
kutoka kwa vikosi vya Kikurdi.
Aidha
wanaharakati wanasema wakaazi kadhaa wameuwawa mjini humo kufuatia
mashambulio ya angani katika eneo la Kaskazini huku shirika la kimataifa
la kutetea haki za binaadamu Amnesty International likisema muungano
unaoongozwa na Marekani lazima ufanye kila juhudi kuzuwiya mauaji ya
raia. DW
SHARE
No comments:
Post a Comment