Jumuiya ya Umoja wa Wanawake
Tanzania (UWT) inaunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais Dkt John Pombe
Magufuli na kupongeza jitihada zake za kupambana na aina zote za
ubadhirifu, dhulma na unyonyaji uliobainika kwenye mikataba ya uchimbaji
na usafirishaji madini, na hivyo kuhakikisha maliasili za Taifa
zinatumika kwa manufaa ya watanzania wote.
Pia, Umoja wa Wanawake
Tanzania unatoa pongezi kwa wajumbe wa Kamati kwa weledi, uzalendo na
ujasiri mkubwa wa kubainisha hasara kubwa iliyopatikana kwa Taifa letu
kutokana na usafirishaji wa makanikia, na hivyo UWT inakubaliana na
kuunga mkono mapendekezo yote ya Kamati na uamuzi wa Mheshimiwa Rais Dkt
John Pombe Magufuli wa kutaka kurekebisha mikataba na sheria za
usimamizi na uchimbaji wa madini nchini.
Aidha UWT inapongeza hatua za
awali za mazungumzo yaliyofanywa tarehe 14/06/2017 baina ya Mhe
Rais Dkt Magufuli na Mwenyekiti wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation
ambao ni wamiliki wa Kampuni ya Acacia Mining Limited Prof. John L.
Thornton na kukubaliana kuhusu malipo ya fedha zilizopotea na
kushirikiana katika ujenzi wa mtambo wa kuchenjulia dhahabu (smelter)
hapa nchini.
Kufanikiwa kwa mazungumzo
hayo, na marekebisho ya sheria na mikataba ya madini kutawezesha
Watanzania kupiga hatua ya kujikomboa na umasikini, hususani Wanawake
ambao wameendelea kukosa huduma za msingi za kijamii ikiwemo afya,
elimu, maji na malazi bora. Wanawake wengi wanahangaika kwa kukosa
mitaji ya biashara na mikopo ya wajasiriamali wadogo huku wakisumbuliwa
kulipa tozo, ushuru na kodi za kero.
UWT inatoa rai kwa wananchi
wote kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na kujivunia utanzania wetu. Tunamuombea Mhe Magufuli, MwenyeziMungu
azidi kumpa afya njema, moyo wa ujasiri, uzalendo na upendo kwa
watanzania.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI
AMINA MAKILAGI (MB)
KATIBU MKUU
JUMUIYA YA UMOJA WA WANAWAKE TANZANIA.
14/06/2017
SHARE
No comments:
Post a Comment