Polisi nchini Kenya wanasema washambuliaji wamewapiga
risasi na kuwaua watu watatu wakati wa uvamizi wa benki moja ya
kibiashara kaskazini mashariki mwa nchi hiyo hivi leo.
Waliouawa ni raia wawili na afisa mmoja wa polisi katika mashambulizi
hayo kwenye Kaunti ya Mandera, kwa mujibu wa kamanda wa polisi, Charles
Chacha."Kulikuwa na majambazi watano wenye silaha. Walipofika kwenye benki, walimpiga risasi afisa wa polisi aliyekuwapo mlangoni, na polisi walifanikiwa kumpiga risasi mmoja wa wahalifu hao, lakini...walikimbia," Chacha aliliambia shirika la habari la Reuters.
Elwak, mahala hasa ambapo mashambulizi hayo yametokea, pako karibu na mpaka wa Somalia.
Shirika la kimataifa la Msalaba Mwekundu linasema pia kuwa bomu lililotegwa barabarani limeripuka kwenye mji huo huo wa Mandera, ingawa hakuna taarifa za waliouawa ama kujeruhiwa kwenye mripuko huo.
Mandera imekuwa ikishuhudia mashambulizi ya mara kwa mara, ambayo yameangamiza maisha ya maafisa kadhaa wa usalama na raia wa kawaida.
Kundi la kigaidi la al-Shabaab lenye mafungamano na al-Qaida limekuwa likibeba dhamana ya mashambulizi hayo.
SHARE
No comments:
Post a Comment