Rais wa zamani wa Botswana, Ketumile Masire, amefariki
dunia katika hospitali moja kwenye mji mkuu wa nchi yake, Gaborone,
akiwa na umri wa miaka 91, baada ya kuuguwa kwa zaidi ya mwezi mmoja.
"Ameondoka duniani kwa amani katika hospitali ya binafsi ya Bokamaso
akiwa amezungukwa na familia yake majira ya saa 4:20 tarehe 22 Juni
2017", alisema msaidizi wake mkuu, Fraser Tihoiwe, kwenye taarifa yake
kwa vyombo vya habari iliyotolewa leo (Ijumaa, 23 Juni), akiongeza
kwamba familia yake inawashukuru watu wote kwa kuwafariji. Masire, ambaye hadi katika siku za hivi karibuni alikuwa akihusika sana kwenye jitihada za kumaliza mapigano kati ya serikali ya Msumbiji na chama cha upinzani cha Renamo akiwa mwenyekiti mwenza wa kundi la kimataifa la wapatanishi, alilazwa hospitalini hapo tarehe 16 Juni, ambako licha ya kuwekwa chumba cha wagonjwa mahututi, familia yake inasema alikuwa akiendelea vyema.
Mbali ya kuwa mpatanishi wa mzozo wa Msumbiji ambako Renamo ilikata kuyatambua matokeo ya uchaguzi wa mwaka 2014 iliposhindwa tena na Frelimo na hivyo kuzusha ghasia mpya nchi nzima mwaka jana, Masire alisaidia pia kwenye kutatua mizozo ya kisiasa nchini Kenya na Lesotho, akiwa mmoja wa viongozi wakongwe wa Afrika wanaoheshimiwa sana.
Alikuwa pia mwenyekiti wa Jopo la Wazee wa Busara waliochunguza mazingira ya mauaji ya maangamizi ya mwaka 1994 nchini Rwanda.
Masire aliingia madarakani mwaka 1980 kufuatia kifo cha Rais Seretse Khama hadi alipoondoka mwenyewe mwaka 1998, akiwa amesimamia kipindi cha ukuwaji mkubwa sana wa kiuchumi.
Anachukuliwa kama ndiye muasisi wa uthabiti wa kiuchumi na kisiasa wa Botswana.
Ikiwa moja ya nchi zenye uthabiti mkubwa barani Afrika, Botswana ni jamhuri ambayo chama cha Masire kiitwacho Bechuanaland Democratic Party (BDP) kimekuwa madarakani tangu uhuru wake mwaka 1966.
CHANZO: DW
SHARE
No comments:
Post a Comment