NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR
NAIBU
Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt. Abdulla Juma Saadalla ‘Mabodi’ ameshiriki
katika mazishi ya watoto wanne waliofariki dunia jana (juzi) baada ya
kuingia kwenye gari iliyokuwa sehemu ya maegesho na likajifunga hali
iliyopelekea watoto hao kukosa hewa na kufariki huko Kidongo Chekundu Unguja.
Marehemu
hao waliotambuliwa kwa majina ya Mwatma Mohamed Malawi (2), Haisam Mustafa(2),
Munawar Ahmed Khamis (3) na Muslim Hamza bakar (2) wote wamezikwa leo katika
maeneo tofauti ya Makaburi ya Mwanakwere na Kiembe samaki Mbuyu Mnene Unguja.
Akizungumza
mara baada ya maziko hayo Naibu Katibu huyo huko katika makaburi ya
Mwanakwerekwe, alisema CCM imepokea kwa masikitiko na mshituko mkubwa taarifa
ya vifo vya watoto hao na inatoa mkono wa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa
familia zilizopata msiba huo na kuwasihi waendelee kuwa wavumilivu kwa kipindi
hiki cha msiba huo.
Alisema
watoto hao walitarajiwa kuwa ni miongoni mwa viongozi na wataalamu wa fani
mbali mbali wa baadae hivyo msiba huo umeacha pengo kubwa kwa familia na
taifa kwa ujumla.
Aidha
Dkt. Mabodi aliwataka wazazi na walezi nchini kuwa karibu na watoto wao kwa
kuhakikisha mazingira yanayotumiwa na watoto kucheza yanakuwa katika hali ya
usalama ili kuepuka athari zinazoweza kusababisha majeraha ama vifo kwa watoto
wao.
“ Kwa
niaba ya CCM Zanzibar nawaomba wanafamilia wote wawe wavumilivu kwa kipindi
hichi cha msiba huku vyombo vya ulinzi na usalama vikiendelea kufanya uchunguzi
wa kina juu ya kubaini chanzo halisi cha vifo hivi na kutoa taarifa kwa umma.”,
alisema Dkt. Mabodi.
Wakizungumza
kwa nyakati tofauti baadhi ya ndugu na wazazi wa marehemu hao walifafanua kuwa
(jana) juzi majira saa 5:00 asubuhi watoto hao walikuwa wakicheza katika maeneo
ya nyumbani kwao ghafla hawakuonekana mtaani hali iliyozusha hofu kwa familia
za watoto wao na wakachukua juhudi za kuwatafuta katika maeneo mbali mbali hasa
katika bandari na maeneo mengine kwa kuhofia kuwa wameibiwa na watu
wasiojulikana.
Akieleza
zaidi Bw. Ahmed Khamis ambaye ni baba mzazi wa mtoto aliyefariki ambaye
ni Munawar, alidai kuwa katika harakati za kuwatafuta watoto hao walifanikiwa
kuwapata majira ya saa 2:00 usiku wa july 16, Mwaka huu wakiwa ndani ya
gari moja lililokuwa limeegeshwa katika maegesho ya gari za mtaani ambalo
mmiliki wake aliliweka kwa muda mrefu na alikuwa amesafiri.
Bw.
Ahmed alieleza kwamba baada ya hapo yeye kwa kushirikiana na majirani mbali
mbali walishirikiana kuvunja milango ya gari hilo na kufanikiwa kuwatoa watoto
hao wakiwa wamezimia na kupelekwa hospitali kuu yaMnazi Mmoja ambapo baada ya
kufanyiwa vipimo na madaktari wakaambiwa kuwa tayari wamefariki dunia kutokana
na kukosa hewa kwa muda mrefu.
Kwa
mujibu wa maelezo ya shuhuda mmoja aliyehusika na harakati za kuwatoa watoto
ndani ya gari walipokutwa wamefariki alisema mazingira yake yanaonyesha kuwa
kabla ya watoto hao kufariki walikuwa wakichezea gari hilo na walipoingia ndani
mlango ulijifunga na kushindwa kutoka nje hali iliyosababisha kukosa hewa na
kufariki dunia.
Viongozi
mbali mbali wa serikali na Chama Cha Mapinduzi waliudhuria katika mazishi hayo
wakiwemo Katibu wa Kamati Maalum, Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar, Bi.
Waride Bakari Jabu, Mbunge wa Jimbo la Jang’ombe Ali Hassan Omar ‘King’
na Waziri wa Kazi,uwezeshaji, wazee, vijana wanawake
na watoto Maudline Castico.
SHARE
No comments:
Post a Comment