TRA

TRA

Sunday, August 27, 2017

Ni viongozi wangapi Afrika wanahimili anachosema JK?

Share On Facebook ! Tweet This ! Share On Google Plus ! Pin It ! Share On Tumblr ! Share On Reddit ! Share On Linkedin ! Share On StumbleUpon !



Julian Msacky

“Kama ni kweli tunapenda amani kama viongozi wanavyosema kwa nini bara letu limezungukwa na vita?”.

Alihoji hivyo Rais mstaafu wa Nigeria, Olusegun Obasanjo wakati akizungumza katika mkutano wa Jukwaa la Viongozi Afrika maarufu kama The Africa Leadership Forum (ALF). 

Obasanjo hakuishia hapo bali alionesha masikitiko yake namna Libya ilivyotumbukia kwenye vita na amani haijapatikana hadi leo.

Ni kwa nini Rais huyo anahoji hivyo? Hili ni swali muhimu kwa sababu viongozi wa Afrika wamekuwa mabingwa wa kuhubiri amani na upendo kwa shingo upande.

Matokeo yake wanaingiza mataifa yao kwenye vita visivyokwisha. Chanzo kikubwa cha machafuko ni wanasiasa wenyewe, lakini waathirika ni raia.

Kwa sababu hiyo wanahubiri amani na mikononi wamebeba majambia ya kubaki madarakani hata kwa kumwaga damu. 

Hawapo tayari kushindwa hata kwa sanduku la kura. Ndiyo maana leo hii wananchi wakisikia kitu kinachoitwa uchaguzi mioyo yao inashtuka.

Ndiko viongozi wa Afrika walikofikisha raia wao. Hii ikiwa na maana kuwa kipindi cha uchaguzi ni kipindi cha hofu.

Hii ni kwa sababu wananchi huweka mguu sawa ili wajue pa kukimbilia kwani ghasia zinaweza kuibuka wakati wowote.

Hii ndiyo Afrika ambayo viongozi wake hujigamba ni walezi wazuri wa demokrasia, utawala bora na sheria.

Lakini matokeo yake wanatumia nyundo kufifisha mifumo hiyo kwa kisingizio cha kulinda amani wakati si kweli.

Ni kwa sababu hiyo Rais mstaafu, Jakaya Kikwete alitumia mkutano huo uliofanyika Johannesburg, Afrika Kusini kuwakumbusha viongozi umuhimu wa kutojenga chuki na vyama vya upinzani.

Kikwete ambaye anasifiwa kwa kutoa fursa kubwa kwa wapinzani kusema, aliwaambia viongozi wa vyama tawala barani Afrika kwamba upinzani ni ufunguo wa demokrasia.

Hakuishia hapo bali aliendelea kusisitiza kuwa viongozi waliopo madarakani watakuwa wanafanya makosa kwa kuwachukulia wapinzani kama maadui.

Kusema kweli hizi ni nasaha muhimu kwa viongozi wa bara letu kwa sababu bila kulea vyama hivyo badala ya amani ni vurugu. 

Badala ya demokrasia ni utawala wa mabavu. Badala ya utawala bora na sheria ni maangamizi.  

Kwa kutozingatia ukweli huo mchungu Afrika imejikuta ikingia kwenye machafuko ya mara kwa mara kwa sababu baadhi ya viongozi wana shingo ngumu.

Swali sasa ni je, ni viongozi wangapi Afrika wanahimili anachosema Kikwete kwa ustawi wa Afrika na watu wake?.
 Rais mstaafu Jakaya Kikwete

Viongozi waliopo madarakani ni muhimu kuzingatia ushauri wa Kikwete kwani una maslahi mapana zaidi kwa Afrika.

Tabia ya viongozi waliopo madarakani kujiona wao ndiyo alfa na omega, ni kujidanganya na kushindwa kusoma alama za nyakati.

Hivi haikuandikwa kwamba ajikwezaye atashushwa na ajishushae atakwezwa?
Au haikusema kwamba mkiwapenda wale mnaowapenda tu mwapata thawabu gani?

Kwa msingi huo viongozi wa Afrika ni lazima wajenge mfumo wa kuendesha siasa kwa njia ya kuvumiliana.

Wajifunze kuendesha siasa kwa kutoa pia fursa kwa wengine ili sauti zao zisikike kwani ndivyo tangazo la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa linavyotaka.

Historia inaonesha kwamba kutoa fursa kwa raia au asasi nyingine za kijamii kutoa hisia zao inajenga zaidi kuliko kubomoa.

Ndiyo maana Waziri Mkuu akiwa Tabora aliwataka viongozi wasizue wananchi kutumia mabango kwani wanatoa hisia zao/kuwasilisha matatizo yao. 

Huo ndiyo ukomavu wa kisiasa na siasa maana yake ni pamoja na kuhimili changamoto/upinzani kutoka kwa wadau wengine.

Ni imani ya Waafrika na Watanzania kwa ujumla kwamba ujumbe wa Kikwete utakuwa chachu ya kupanua wigo wa demokrasia katika bara letu la Afrika.

“Utawala bora bila serikali imara ni jambo lisilowezekana,” alisema Kikwete na kuhimiza uwepo uwiano sawa kwa wabunge kutoa hoja zao.

Afrika ambayo inapitia changamoto nyingi za ujio wa mfumo wa vyama vingi vya siasa ni lazima ijifunze namna ya kuendesha mfumo huo bila kuumiza wengine.

Ili Afrika ibaki salama chini ya mfumo huo sharti mfumo wa utawala bora na sheria uheshimiwi ili kurutubisha demokrasia.

Ni lazima pia uwepo uvumilivu wa kweli kisiasa badala ya kujengeana chuki na uhasama bila sababu za msingi.




Author:

«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post

No comments:

Post a Comment

 
Copyright ©2016 NCHI YANGU • All Rights Reserved.
Template Design by AT Creatives • Powered by Blogger